Home » » WAWEKEZA TRILIONI 4/- KATIKA MBOLEA

WAWEKEZA TRILIONI 4/- KATIKA MBOLEA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com Imeandikwa na Matern Kayera
Mkurugenzi wa Kituo cha Uwekezaji nchini (TIC), Geoffrey Mwambe
KITUO cha Uwekezaji Tanzania (TIC) jana kimepokea nyaraka za maombi ya usajili wa kampuni za kuzalisha mbolea ambazo uwekezaji wake una thamani ya dola za Marekani bilioni 1.9 ambazo ni sawa na zaidi ya Sh trilioni 4.
Kampuni hizo ni Ferrostaal kutoka Ujerumani na Haldor Topsoe ya Denmark ambazo zimekuja kuwekeza katika uzalishaji wa mbolea ya chumvi katika eneo la Kilwa Masoko mkoani Lindi.
Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi Mtendaji wa TIC, Geoffrey Mwambe wakati wa hafla fupi ya upokeaji wa nyaraka za usajili wa mradi huo. Alisema mradi huo wa mbolea utatumia rasilimali ya gesi asilia inayopatikana hapa nchini katika shughuli zake za uzalishaji na utakuwa ukizalisha tani milioni 1.3 za mbolea kwa mwaka.
“Mbali na kiwango cha tani milioni 1.3 za mbolea zitakazokuwa zikizalishwa kila mwaka, mradi huo pia utaajiri Watanzania 4,500 na wageni 300,” alisema Mwambe. Akifafanua zaidi kuhusu mradi huo, Mwambe alisema kuwa mradi huo utasajiliwa hapa nchini kwa jina la Tanzania Mbolea Petrochemicals (TAMCO).
“TIC tutasimamia na kuhakikisha kila taasisi inayohusika na utoaji wa vibali kama vile vinavyohusu mazingira au vibali vya kufanya kazi na ukaazi kwa ajili ya wataalamu wa kufunga mitambo na mashine vinapatikana kwa wakati ili kampuni itumie muda mfupi kujenga kiwanda chake na sisi tuanze kuona mapema matunda ya mradi huu,” alisema Mwambe.
Mwambe alisema ukubwa wa mradi ni ujumbe tosha kwa wawekezaji mbalimbali duniani kwamba Tanzania ni mahali panapofaa kwa uwekezaji kwa kuwa kuna mazingira rafiki, serikali inayoaminika na kuwepo kwa mfumo unaosaidia kupata uwekezaji mwingi.
Alisema uwekezaji huo ni kichocheo kikubwa katika ukuaji wa sekta ya viwanda lakini pia kwa kipindi kirefu kumekuwa na changamoto katika sekta ya kilimo kutokana na kiasi kikubwa cha mbolea kuagizwa kutoka nje, jambo ambalo kiuchumi halina afya.
“Kuzalisha mbolea hapa nchini kwa kutumia rasilimali zetu, ina maana kuwa mbolea itakuwa inapatikana kwa wakati, itawafikia wakulima kwa urahisi na bei nafuu na kupunguza matumizi ya fedha za kigeni zilizokuwa zikitumika kuagiza mbolea kutoka nje, lakini pia itaunganisha sekta nyingine za kiuchumi,” alisema Mwambe.
Mwambe alisema mradi huo utasaidia kupunguza tatizo la upatikanaji wa mbolea nchini kwa kuwa mahitaji halisi ya bidhaa hiyo ni zaidi ya tani 350,000. Huu ni uwekezaji mkubwa katika uzalishaji wa pembejeo za kilimo hapa nchini na kuwa uzaishaji wake utapunguza mahitaji ya mbolea ambayo ni tani lakini 3.5.
Kiwanda cha mbolea cha Minjingu huzalisha tani 100,000 kwa mwaka ikiwa ni wastani wa asilimia 20 ya mahitaji yote. Kwa upande wake msimamizi wa mradi huo hapa nchini, Wilfread Wineam alisema kuwa kiwanda hicho kina uwezo wa kuzalisha tani milioni 1.3 kwa mwaka na asilimia 30 ya mbolea itauzwa hapa nchini na itakayobaki itauzwa nje ya nchi.
Naye Balozi wa Ujerumani hapa nchini, Detlet Waecheter alisema kutokana na dira ya Tanzania ya kuwa na uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025, hivyo uwekezaji wa moja kwa moja wa kigeni nao ni muhimu katika kufikia malengo hayo.
Alisema kuwa uwekezaji wa kiwanda cha mbolea ni mwanzo kwa wawekezaji wengine wengi kuja kuwekeza Tanzania na kuahidi kuleta ujumbe mkubwa wa wawekezaji kutoka Jimbo la Bavaria ili kuja kujionea fursa mbalimbali za uwekezaji.
Aidha, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Mbolea ya Minjingu iliyopo mkoani Manyara, Pardeep Singh Hans alisema kuwa ni vyema mradi huu ukatekelezwa kwa haraka ili kukamata soko la bidhaa hiyo mapema.
CHANZO HABARI LEO
hatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Lindi Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa