NAIBU WAZIRI WA MADINI MHE BITEKO AWATAKA WACHIMBAJI WADOGO WA GYPSUM KUWA NA UMOJA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Naibu Waziri wa Wizara ya Madini Mhe Dotto Mashaka Biteko akiwasili kijiji cha Hoteli Tatu, Kata ya Mandawa Wilaya ya Kilwa Mkoani Lindi kwa ajili ya kuembelea kampuni ya Universal Mining Ltd kujionea hali ya uzalishaji wa jasi (Gypsum) unavyoendelea wakati wa ziara ya Siku tatu katika Mkoa wa Lindi na Mtwara, Leo 17 Januari 2018. Picha Zote Na Mathias Canal
Naibu Waziri wa Wizara ya Madini Mhe Dotto Mashaka Biteko  akikagua uzalishaji wa madini aina ya Jasi (Gypusm) katika kijiji cha Hoteli Tatu, Kata ya Mandawa Wilaya ya Kilwa Mkoani Lindi, Leo 17 Januari 2018.
Naibu Waziri wa Wizara ya Madini Mhe Dotto Mashaka Biteko  akizungumzia umuhimu wa wachimbaji wadogo kuwa na umoja ili kukuza ufanisi na tija katika kupanga bei ya rasilimali wanazozalisha wakati alipozuru kijiji cha Hoteli Tatu, Kata ya Mandawa Wilaya ya Kilwa Mkoani Lindi, Leo 17 Januari 2018.

Na Mathias Canal, Lindi

Naibu Waziri wa Wizara ya Madini Mhe Dotto Mashaka Biteko Leo 17 Januari 2018 amewataka wachimbaji wadogo wa madini Jasi(Gypsum) kuwa na umoja na mshikamano katika uuzaji madini hayo na kuwa na kauli moja katika ushiriki wa soko la bidhaa hiyo.

Mhe Biteko ameyasema hayo alipotembelea katika kijiji cha Hoteli Tatu, Kata ya Mandawa Wilaya ya Kilwa Mkoani Lindi wakati wa ziara ya Siku tatu katika Mkoa wa Lindi na Mtwara ambapo pamoja na mambo mengine atakutana na makundi ya wachimbaji wadogo ili kubaini changamoto zao na kuzitafutia ufumbuzi.

Alisema kuwa kila mchimbaji anajipangia gharama aitakayo yeye pasina kushirikiana na wachimbaji wengine ili kuwa na bei moja ambayo itakuwa na tija na manufaa kwa kila mmoja hivyo kupitia umoja wao watakuwa na kauli na maamuzi ya pamoja yenye tija na faida kwao.

Mhe Biteko aliwashauri wachimbaji hao kuwa na umoja utakaokuwa na uwezo wa kudai bei itakayofanana kwa wote pia kuwa na uwezo wa kutengeneza sheria ndogondogo ambazo zitatumika kujisimamia wao wenyewe.

Aidha, amezitaja Changamoto mbalimbali zinazowakabili wananchi sambamba na wachimbaji wadogo hususani ubovu wa barabara ambapo ameishauri Ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa kusaidia utengenezaji wa Barabara itakayorahisisha usafirishaji wa jasi (Gypusm) na kurahisisha huduma za wananchi ili kufika kwa urahisi katika Barabara kuu.

Mhe Biteko alisema kuwa serikali ya awamu ya Tano chini ya Rais Dkt John Pombe Magufuli itaendelea na juhudi zake za kuweka miundombinu rafiki kwa ajili ya wananchi, wawekezaji, na wachimbaji (wakubwa na wadogo) hivyo ili kufikia adhma ya mafanikio hayo ni lazima kusema na kutekeleza maelekezo yote ili kupiga hatua za maendeleo.

Alibainisha kuwa nia ya sekta ya madini ni kufanya mchakato wa kuongeza pato la Taifa kufikia asilimia 10% tofauti na ilivyo hivi sasa ambapo sekta ya madini inachangia kiasi kidogo kwenye pato la Taifa.


SERIKALI KUTOA MUONGOZO WAS UTOAJI TIBA KWA HOSPITALITY NCHINI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Na.WAMJW,Ruangwa.

Wizara ya Afya,Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wazee na watoto inatarajia kutoa mwongozo wa utoaji tiba kwenye hospitali zote nchini ili kuwe na mfumo mzuri wa dawa muhimu ili kuepusha madaktari kuagiza dawa ambazo zipo nje ya mfumo wa dawa muhimu.

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Afya Dkt.Faustine Ndugulile wakati wa ziara yake ya kuangalia hali ya upatikanaji wa dawa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya vya Serikali .

“Kabla ya mwisho wa mwaka tunataka kutoa muongozo huo(Standard Treatment Guidline) kwa sababu imekua changamoto kwani wale wauzaji wakubwa wa dawa wamekua wakizitembelea hospitali kubwa na kuwarubuni wanunue dawa zao ambazo zipo nje ya dawa zetu muhimu”

Kwahiyo muongozo huo itakua kila ugonjwa dawa ya kwanza itakua ipi na kama itashindika dawa itakayofuata dawa ipo na hizo dawa zitaagizwa na kutunzwa na Bohari ya Dawa(MSD).

Hata hivyo Dkt.Ndugulile amewataka watendaji wa hospitali hiyo kuweka utaratibu na mpangilio mzuri na unaohitajikwa wa utunzaji wa dawa kwenye stoo ya madawa iliyopo hospitalini hapo,baada ya kukuta hakuna upangaji mzuri wa dawa na vifaa tiba “mmenithibitishia kwamba dawa zote mnazipata kwa asilimia 90 hivyo ni vyema Mfamasia wa Wilaya kuzipanga dawa hizo vizuri na kuweka kiyoyozi ambacho kitasaidia kutunza dawa kwa muda bila kuharibika”

Alisema hivi sasa nchi haina tatizo la upatikanaji wa dawa kwani bajeti ya dawa hivi sasa imeongezeka kutoka shilingi bilioni 30 mpaka zaidi ya bilioni 260 kwa mwaka huu wa fedha “bajeti hii imekua ikitolewa na Mhe.Rais amekua akizitoa fedha zote,hivyo hatuna shida ya fedha hivyo nasi hatutarajii kuwa na shida ya dawa na dawa tunazokuwa tunazipata zitunzwe vizuri”.

Aidha,amezitaka kamati za afya katika ngazi za zahanati,vituo vya afya na hospitali zinafanya kazi ipasavyo kwa kusimamia matumizi mazuri ya dawa.

Kwa upande wa ubora wa huduma za afya kwa vituo vya kutolea huduma za afya vya serikali hivyo kumekua na mkakati wa kuwa na ubora wa vituo vya serikali kwa kuwapatia nyota kulingana na ubora uliopo kwenye vituo kwa kuangalia utoaji wa huduma,maabara na sehemu zingine za kutolea huduma.

Kwa upande wa Mfuko wa afya wa jamii(CHF) Dkt.Ndugulile amewapongeza wilaya hiyo kwa kusajili kaya 13,788 kutoka 978 mwaka 2016/2017,ambapo wamewapatia vitambulishovya matibabu wazee 4,000.“hivi sasa Serikali inataka kuwa na bima kwa wote kwani gharama ya matibabu kwa sasa ni kubwa sana hasa na kumekua na ongezeko la magonjwa yasiyo ya kuambukizwa,hivyo tunataka kuwasaidia wananchi ambao hawawezi kumudu gharama hizo ili anavyokwenda kwenye vituo vyetu asiwaze masuala ya kutoa fedha”alisema Dkt.Ndugulile.

Akisoma ripoti ya Wilaya hiyo Kaimu Mganga Mkuu wa Wilaya hiyo Dkt. Ernest Ntahuka Alisema Halmashauri hiyo imeweza kuboresha hali ya upatikanaji wa dawa kwa asilimia 85 kutoka asilimia 60 ya mwaka 2015/2016.Hata hivyo alisema Halmshauri ya Ruangwa kwa mwaka 2017/2017 imetenga shilingi milioni 650 kwa ajili ya ujenzi wa hospitali mpya ya wilaya na tayari imeshatenga eneo la ujenzi lenye ukubwa wa hekari 60 ambapo ramani ya ujenzi huo tayari imeandaliwa

WAWEKEZA TRILIONI 4/- KATIKA MBOLEA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com Imeandikwa na Matern Kayera
Mkurugenzi wa Kituo cha Uwekezaji nchini (TIC), Geoffrey Mwambe
KITUO cha Uwekezaji Tanzania (TIC) jana kimepokea nyaraka za maombi ya usajili wa kampuni za kuzalisha mbolea ambazo uwekezaji wake una thamani ya dola za Marekani bilioni 1.9 ambazo ni sawa na zaidi ya Sh trilioni 4.
Kampuni hizo ni Ferrostaal kutoka Ujerumani na Haldor Topsoe ya Denmark ambazo zimekuja kuwekeza katika uzalishaji wa mbolea ya chumvi katika eneo la Kilwa Masoko mkoani Lindi.
Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi Mtendaji wa TIC, Geoffrey Mwambe wakati wa hafla fupi ya upokeaji wa nyaraka za usajili wa mradi huo. Alisema mradi huo wa mbolea utatumia rasilimali ya gesi asilia inayopatikana hapa nchini katika shughuli zake za uzalishaji na utakuwa ukizalisha tani milioni 1.3 za mbolea kwa mwaka.
“Mbali na kiwango cha tani milioni 1.3 za mbolea zitakazokuwa zikizalishwa kila mwaka, mradi huo pia utaajiri Watanzania 4,500 na wageni 300,” alisema Mwambe. Akifafanua zaidi kuhusu mradi huo, Mwambe alisema kuwa mradi huo utasajiliwa hapa nchini kwa jina la Tanzania Mbolea Petrochemicals (TAMCO).
“TIC tutasimamia na kuhakikisha kila taasisi inayohusika na utoaji wa vibali kama vile vinavyohusu mazingira au vibali vya kufanya kazi na ukaazi kwa ajili ya wataalamu wa kufunga mitambo na mashine vinapatikana kwa wakati ili kampuni itumie muda mfupi kujenga kiwanda chake na sisi tuanze kuona mapema matunda ya mradi huu,” alisema Mwambe.
Mwambe alisema ukubwa wa mradi ni ujumbe tosha kwa wawekezaji mbalimbali duniani kwamba Tanzania ni mahali panapofaa kwa uwekezaji kwa kuwa kuna mazingira rafiki, serikali inayoaminika na kuwepo kwa mfumo unaosaidia kupata uwekezaji mwingi.
Alisema uwekezaji huo ni kichocheo kikubwa katika ukuaji wa sekta ya viwanda lakini pia kwa kipindi kirefu kumekuwa na changamoto katika sekta ya kilimo kutokana na kiasi kikubwa cha mbolea kuagizwa kutoka nje, jambo ambalo kiuchumi halina afya.
“Kuzalisha mbolea hapa nchini kwa kutumia rasilimali zetu, ina maana kuwa mbolea itakuwa inapatikana kwa wakati, itawafikia wakulima kwa urahisi na bei nafuu na kupunguza matumizi ya fedha za kigeni zilizokuwa zikitumika kuagiza mbolea kutoka nje, lakini pia itaunganisha sekta nyingine za kiuchumi,” alisema Mwambe.
Mwambe alisema mradi huo utasaidia kupunguza tatizo la upatikanaji wa mbolea nchini kwa kuwa mahitaji halisi ya bidhaa hiyo ni zaidi ya tani 350,000. Huu ni uwekezaji mkubwa katika uzalishaji wa pembejeo za kilimo hapa nchini na kuwa uzaishaji wake utapunguza mahitaji ya mbolea ambayo ni tani lakini 3.5.
Kiwanda cha mbolea cha Minjingu huzalisha tani 100,000 kwa mwaka ikiwa ni wastani wa asilimia 20 ya mahitaji yote. Kwa upande wake msimamizi wa mradi huo hapa nchini, Wilfread Wineam alisema kuwa kiwanda hicho kina uwezo wa kuzalisha tani milioni 1.3 kwa mwaka na asilimia 30 ya mbolea itauzwa hapa nchini na itakayobaki itauzwa nje ya nchi.
Naye Balozi wa Ujerumani hapa nchini, Detlet Waecheter alisema kutokana na dira ya Tanzania ya kuwa na uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025, hivyo uwekezaji wa moja kwa moja wa kigeni nao ni muhimu katika kufikia malengo hayo.
Alisema kuwa uwekezaji wa kiwanda cha mbolea ni mwanzo kwa wawekezaji wengine wengi kuja kuwekeza Tanzania na kuahidi kuleta ujumbe mkubwa wa wawekezaji kutoka Jimbo la Bavaria ili kuja kujionea fursa mbalimbali za uwekezaji.
Aidha, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Mbolea ya Minjingu iliyopo mkoani Manyara, Pardeep Singh Hans alisema kuwa ni vyema mradi huu ukatekelezwa kwa haraka ili kukamata soko la bidhaa hiyo mapema.
CHANZO HABARI LEO
hatsapp namba +255765056399.

‘RUANGWA INAHITAJI SEKONDARI YA WASICHANA’-WAZIRI MKUU KASSIM MAJALIWA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
 Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akikagua ujenzi wa shule ya msingi Ng’au, katika kata ya Mnacho, Wilayani Ruangwa, alipokuwa kwenye ziara ya kikazi ya siku moja Wilayani Ruangwa, Novemba 5, 2017. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
  Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza na wananchi mara baada ya kukagua ujenzi wa shule ya msingi Ng’au, iliyopo kata ya Mnacho Wilayani Ruangwa, Novemba 5, 2017.
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akimpongeza mwenyekiti wa Kamati ya Ujenzi wa Shule ya msingi Ng’au iliypo Wilayani Ruangwa, Daniel Chilemba kwa kusimamia ujenzi kikamilifu, wakati alipoenda kukagua ujenzi wa shule, Novemba 5, 2017.
 
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema wilaya ya Ruangwa inahitaji kuwa na shule ya sekondari ya wasichana ambayo ni ya bweni ili kupunguza tatizo la wasichana kukosa elimu.

Ametoa wito huo jana (Jumapili, Novemba 5, 2017) wakati akizungumza na wakazi wa kijiji cha Ng’au, kata ya Mnacho wilayani Ruangwa mkoani Lindi ambako alienda kukagua ujenzi wa shule mpya ya msingi ambayo ujenzi wake ulianza wiki mbili zilizopita.

“Mpango wetu ni kujenga shule ya msingi mpya hapa kijijini Ng’au ili watoto wanaotoka ng’ambo hii wasome hapa hapa. Wakati wa masika nyote mnajua taabu wanayopata watoto wetu kukatisha kwenda ng’ambo ile,” alisema.

“Nimefurahi kukuta msingi wa vyumba tisa uko tayari na hii idadi inaweza kuongezeka. Wanakijiji tushirikiane kujaza kifusi ili kazi ya ujenzi iende haraka,” alisema.Waziri Mkuu alisema ng’ambo ya pili kuna shule ya msingi Mnacho ambayo ina madarasa 11 na wanafunzi waliopo ni karibu 500, na ndoto yake ilikuwa ni kuona ile shule inabadilika na kuwa ya sekondari.

“Ile shule ina historia na wakazi wengi kutoka Nandagala, Namahema, Chimbila ‘A’ na Chiemeka wamesoma pale. Mimi mwenyewe nimesoma pale kuanzia darasa la kwanza hadi la saba. Shule ilishazeeka, ndipo tukatafuta fedha ili ifanyiwe ukarabati na sasa ina miundombinu mizuri ndiyo sababu inaonekana inafaa kuwa ya sekondari,” alisema.

“Kwa vile shule ina miundombinu ya kutosha, ni vema ikawa ya bweni ambayo ni mahsusi kwa wasichana wa wilaya hii kwani tunalo tatizo la watoto wa kike kupata elimu, na wanahangaika sana,” alisema.

“Ujenzi wa hii shule ukikamilika, watoto wale 500 watahamia hapa na walimu wao na ile pale itapokea wanafunzi sekondari za wilaya hii ili tuwe na kidato cha kwanza hadi cha nne na ianze mara moja,” alisema.

Alisema shule hiyo itaitwa Lucas Malia kwa heshima ya mwalimu mkuu wa zamani wa shule hiyo ambaye alisomesha watu wengi katika wilaya hiyo na wengine sasa hivi ni viongozi Serikalini na jeshini. Mwalimu Malia hivi sasa ni marehemu.

Waziri Mkuu amerejea Dodoma leo asubuhi kuendelea na vikao vya Bunge vinavyotarajiwa kuanza kesho (Jumanne, Novemba 7, 2017).


IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
S. L. P. 980,
40480 - DODOMA.
JUMATATU, NOVEMBA 6, 2017.
 

WAZIRI MKUU AWAPOKEA WANACHAMA 37 WA UPINZANI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amepokea wanachama wapya 37 kutoka vyama vya CUF na CHADEMA ambao wameamua kurejea Chama cha Mapinduzi (CCM).

Kwa mujibu wa Katibu wa CCM wa wilaya hiyo, Bw. Barnabas Essau wanachama 35 kati ya hao wametoka CUF na wawili wametoka CHADEMA.Wanachama hao walipokelewa jana (Jumapili, Novemba 5, 2017) kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kijiji cha Mbekenyera, wilayani Ruangwa mkoani Lindi.

Bw. Essau alisema wanachama hao wote wametoka kata za Mbekenyela na Matambalale. Walikabidhiwa kadi mpya za CCM, na kula kiapo cha uaminifu.

Akizungumza kwa niaba ya wanachama wenzake wapya, Bw. Mohammed Issa Ndogoro ambaye amehamia kutoka CHADEMA, alisema wamejiunga na CCM baada ya kuridhishwa na mwelekeo wake. Alisema wameguswa na jinsi Serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Dk. John Pombe Magufuli inavyofanya kazi ya kutatua kero za wananchi. 

Alisema amekaa upinzani kwa miaka 23 lakini anaikubali CCM sababu ya uwazi wake na ameshangaa kuona akipewa kadi na stakabadhi ya walipo yenye jina lake, jambo ambalo hajawahi kuliona katika vyama vingine vya upinzani.

“Sote sisi tumehamia CCM, uhai wa chama ni michango. Nani aseme hapa kama aliwahi kupewa stakabadhi katika chama chake, na kama yupo nampa sh. 5,000/- sasa hivi,” alisema Bw. Ndogoro na kuamsha kicheko kwenye mkutano huo.

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
S. L. P. 980,
40480 - DODOMA.
JUMATATU, NOVEMBA 6, 2017.

WAZIRI MKUU AHIMIZA LINDI WAJIPANGE MAANDALIZI YA BARAZA LA MAULID KITAIFA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka wana-Lindi na wana-Ruangwa watumie fursa zilizopo ili kufanikisha maandalizi ya sherehe za Maulid na Baraza la Maulid Kitaifa mwaka huu.
Ametoa wito huo leo (Jumapili, Novemba 5, 2017) wakati akizungumza na viongozi wa dini ya Kiislamu wa Mkoa wa Lindi na wilaya ya Ruangwa mara baada ya kuwasili wilayani humo kwa ziara ya siku moja.
Waziri Mkuu amesema sherehe hizo zitafanyika Desemba mosi kwa mkesha wa Maulid na kufuatiwa na Baraza la Maulid litakalofanyika Desemba 2, saa 3 asubuhi kwenye viwanja vya shule ya msingi Likangale.
Aliwataka wana-Ruangwa waharakishe kujenga nyumba za kulala wageni na sehemu za kula ili waweze kupokea ugeni huo mkubwa wa kitaifa. “Kila mmoja anayeona hapo kuna fursa, ni lazima aitumie vizuri,” alisisitiza.
“Kwa niaba ya wana-Ruangwa, tunamshukuru Mheshimiwa Mufti na Baraza la Maulamaa kwa kuridhia sherehe hizi zifanyike kitaifa hapa wilayani kwetu. Nitumie fursa hii kuwaomba Waislamu wote tuungane katika sherehe hizi licha ya tofauti za madhehebu yetu tuliyonayo,” alisema.
Alisema uamuzi huo wa BAKWATA ulitangazwa kwenye Baraza la Maulid lililofanyika Singida, mwaka jana ya kwamba wameamua kuadhimisha sherehe hizo kwenye ngazi ya wilaya badala ya kuwa inafanyika makao makuu kila mwaka.
Waziri Mkuu alitumia fursa hiyo kuwaarifu viongozi hao kwamba maandalizi yanaendelea na kwamba vifaa mbalimbali kama mchele, vitoweo, unga wa ngano, sukari, maji, juisi, mahema, mikeka na mazulia vimekwishapatikana.
“Ninaomba Kamati ya Uhamasishaji iifanye kazi hii kwa kutambua kuwa jambo hili si la kwenu peke yenu, bali linaungwa mkono na Serikali, na hii ni kwa sababu Serikali yenu inafanya kazi kwa karibu sana na viongozi wa dini,” alisema.
Alisema misingi ya amani katika nchi hii imejengwa na mahubiri ya viongozi wa dini.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Uhamasishaji, Sheikh Ali Mohammed Mtopa alisema Ruagwa iko tayari na imepokea wito huo wa kitaifa. “Tunakuhakikishia wewe Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na wawakilishi wa Mufti waliopo hapa kwamba tumepokea hiyo heshima,” alisema.
Naye Mkurugenzi wa Itifaki kutoka BAKWATA Makao Makuu na Msimamizi wa Malidi za Kitaifa, Sheikh Mohammad Nassir ambaye alisema wana Ruangwa an wana Lindi wanalo jukumu la kuhamasisha watu washiriki sherehe hizo.
“Hamasa haitatoka Morogoro au Dar es Salaam bali hapahapa Lindi. Tunataraji watu wasiopungua 10,000 watahudhuria sherehe hizi za Maulid kutoka wilaya zote za mkoa wa Lindi na hii ni mbali wawakilishi kutoka kila mkoa wapatao 100 -150,” alisema.
Waziri Mkuu anatembelea vijiji vya jimboni mwake ambako atahutubia wananchi.
IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU, 
JUMAPILI, NOVEMBA 5, 2017.

WATAKAOKWAMISHA MALIPO YA KOROSHO KUKIONA- WAZIRI MKUU MAJALIWA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali itawashughulikia watu wote watakaokwamisha malipo ya wakulima wa zao la korosho.

“Hatutamuacha mtu yeyote atakayesababisha wakulima kuchelewa kulipwa fedha zao. Tutawakamata wote na kuwachukulia hatua stahiki.”

Ametoa kauli hiyo jana (Jumapili, Novemba 5, 2017) alipozungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika Kata ya Mbekenyera wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi.

Waziri Mkuu alisema wakulima hao ni lazima walipwe fedha zao kwa wakati na asitokee mtu wa kuzitamani fedha hizo.

“Mkulima amelima mikorosho mwenyewe, ameokotoa na kukodoa mwenyewe wao wamepewa dhamana ya kuziuza, hivyo wahakikishe wanawapelekea fedha zao na wala wasizitamani.”

Pia Waziri Mkuu amewataka viongozi wa vyama vya Ushirika vya Msingi wahakikishe mkulima hakosi sh. 3,500 katika kilo moja ya korosho atakayoiuza baada ya kukatwa michango.

Alisema bei ya juu ya korosho katika minada ya mkoa wa Lindi sh. ni 3,970 na ya chini sh. 3,800. “Vyovyote itakavyokuwa mkulima hawezi kukosa sh. 3,500, viongozi wa AMCOS mnisikie.”



 Waziri Mkuu alisema hatua hiyo inatokana na kuongezeka kwa bei ya zao la korosho pamoja na kupungua kwa makato ya mkulima ambapo kwa sasa hayazidi sh. 300 katika kilo moja ya korosho.

NAPE AGEUKA MBOGO BAADA YA KUDHIHAKIWA MTANDAONI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Mbunge wa jimbo la Mtama (CCM) Nape Nnauye ameonyesha kukasilishwa na moja ya shabiki katika mtandao wake wa Twitter ambaye amemzihaki na kumwita mnafiki kutokana na ujumbe alioweka, Nape amedai watu wa namna hiyo ni zaidi wa wachawi. 

Leo asubuhi Nape aliweka ujumbe kupitia mtandao wake unaosomeka "Usivunje mtungi kwa sababu ya panya aliyemo ndani ya mtungi, inamisha taratibu, fanya 'timing', utaua panya na mtungi utabaki salama" 
Baada ya kuandika ujumbe huo ndipo moja ya mtu akaja na kumwambia kuwa kiongozi huyo amekua mnafiki baada ya kuvuliwa nafasi ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na kudai kuwa kiongozi huyo amekuwa akiomkosoa boss wake, jambo ambalo Nape Nnauye wiki iliyopita alisema anachukizwa kuona watu wakichukua mambo yako na kuyahusisha na kumsema au kumkosoa Rais jambo ambalo si la kweli. 

"Mkuu we mnafiki sana yote hayo umeanza baaada ya kuvuliwa uwaziri 'come on' kiongozi bora si  yule anaonekana mkosoaji kwa boss wake" aliandika Majdy Wiliam 

WATENDAJI WANAOCHUKUA RUSHWA KWENYE VITUO VYA UKAGUZI WA MAZOA YA MISITU KUKIONA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.



Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Prof Dos Santos Silayo akiwa kwenye mkutano na watendaji wake wa Kanda ya Kusini (hawapo pichani) muda mfupi kabla ya kuwataka meneja kuchukukua hatua kwa watendaji wasio waadilifu mapema hivi leo.
Kaimu Meneja wa Wakala wa Huduma za Misitu Kanda ya Kusini Ebrantino Mgiye (mwenye koti jeusi) akiwasolisha mafanikio na changamoto zinazoikabili kanda huku akifuatiliwa kwa umakini na Meneja Msaidizi wa Mipango na Matumizi Endelevu ya Rasilimali za Misitu Bw. Gaudence Kilasi (aliyekaa) mapema hivi leo.
Baadhi ya Watendaji wa TFS Kanda ya Kusini wakichukua kumbukumbu katika Kikao cha Wafanyakazi kilichoendeshwa na Mtendaji Mkuu wa TFS Prof Dos Santos Silayo kuanza kuzungumza nao mapema hivi leo hii.
Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Prof Dos Santos Silayo akimfuatilia kwa umakini Kaimu Meneja wa Wakala wa Huduma za Misitu Kanda ya Kusini Ebrantino Mgiye (hayupo pichani) alipokuwa akiwasilisha mafanikio na changamoto ya miaka mitatu ya kanda hiyo mapema hivi leo.

Na Tulizo Kilaga Lindi

Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) Prof Dos Santos Silayo amewataka meneja wa misitu nchini kusita kuchukua hatua pale wanapokuwa na ushahidi dhidi ya watendaji wanaojihusisha na vitendo vya rushwa kwenye vituo vya ukaguzi wa mazao ya misitu.

Ametoa agizo hilo leo tarehe 04/10/2017, alipotembelea na kuzungumza na wafanyakazi wa TFS Kanda ya Kusini katika ofisi za Wilaya ya Lindi ya Taasisi hiyo.

“Kuna tuhuma za hovyo nimesikia, watu wanakamatwa na mazao ya misitu yaliyovunwa ama kusafirishwa kinyume na sheria, wanaombwa kitu kidogo na baadhi ya watumishi wasio waaminifu ili kuhalalisha mizigo hiyo na wakigoma, mizigo yao hukamatwa, nataka kuwaona mnachukua hatua stahiki,”amesema.

Mtendaji Mkuu ameeleza kuwa licha ya TFS kuwa na changamoto nyingi anaimani na taasisi hiyo na amewataka watendaji wake kufanya kazi kwa kushirikiana na kamati za ulinzi na usalama za mikoa na wilaya na kuzingatia weledi, uzalendo na uadilifu, akiahidi Serikali kufanyia kazi changamoto zinazowakabili.

Awali, Kaimu Meneja wa Wakala wa Huduma za Misitu Kanda ya Kusini Ebrantino Mgiye alisema miongoni mwa changamoto zinazokabili taasisi hiyo ni pamoja na uhaba wa watendaji.

Hata hivyo, Mtendaji Mkuu amewataka watendaji wa TFS kujikita katika utendaji wa kimkakati ili kuboresha usimamizi na uhifadhi wa raslimali za misitu na Nyuki kwa ajili ya kuchangia katika mahitaji ya kijamii, kiuchumi, ki-ikolojia, na ki-utamaduni kwa kizazi cha sasa na kijacho.


RAIS WA CHAMA CHA WAUGUZI TANZANIA (TANNA) AONGOZA KIKAO CHA WAUGUZI HAO MKOANI LINDI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Rais wa Chama Cha Wauguzi Tanzania (TANNA), Paul Magesa (katikati) akifungua kikao cha kamati ya Mkutano Mkuu wa 45 wa maandalizi ya chama hicho Mkoani Lindi jana. kulia ni Mwenyekiti wa chama cha hicho Mkoa wa Lindi, Patrick Achimpota na Katibu Mkuu wa Chama hicho, Sebastian Luziga. 
Mwenyekiti wa chama cha Wauguzi (TANNA) Mkoa wa Lindi, Patrick Achimpota (kulia), akizungumza jambo wakati wa kikao hicho, kushoto ni Katibu Mkuu wa Chama hicho, Sebastian Luziga na Rais wa Chama Cha Wauguzi Tanzania (TANNA), Paul Magesa.
Viongozi mbalimbali na wajumbe wakisikiliza kwa makini wakati Rais wa Chama cha Wauguzi (TANNA), Paul Magesa alipokuwa akizungumza jambo.
Viongozi na wajumbe wakifuatilia kwa umakini.
Wajumbe wa Mkutano huo wakisikiliza kwa umakini.
Dokt. Sophia Khaify (kulia) akisalimiana na Rais wa Chama cha Wauguzi Tanzania, Paul Magesa mara baada ya kufunga kikao hicho cha Kamati ya Maandalizi jana.
Rais wa Chama cha Wauguzi Tanzania (TANNA), Paul Magesa (kulia) akisalimiana na Mganga Mkuu wa Hospitali ya Mkoa wa Lindi, Ngwechele Makenge, anaye shuhudia katikati ni Makamu wa Rais wa Chama hicho, Ibrahim Mgoo.
Makamu wa Rais wa Chama cha Wauguzi (TANNA), Ibrahim Mgoo (kulia), akisalimiana na Mganga Mkuu wa Hospitali ya Mkoa wa Lindi, Ngwechele Makenge.
Mganga Mkuu wa Hospitali ya Mkoa wa Lindi, Ngwechele Makenge akizungumza jambo na viongozi mbalimbali wa chama cha Wauguzi Tanzania (TANNA), pichani hawapo.
(PICHA ZOTE NA KHAMISI MUSSA).

WAJUMBE MKUTANO MKUU WA 45 CHAMA CHA WAUGUZI TANZANIA (TANNA) SAFARINI LINDI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.



 Wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Chama Cha Wauguzi Tanzania  (TANNA)  kutoka sehemu mbalimbali wakiungana na wajumbe wenzao pamoja na viongozi wa Tanna Mkoa wa Lindi jana katika kufanya maandalizi ya Mkutano Mkutano Mkuu  wa 45 unao tarajiwa kufanyika Oktoba 4-6 Kitaifa  ambapo Mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Mh. Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa.( PICHA ZOTE NA KHAMISI MUSSA)

 Mwenyekiti wa Chama Cha Wauguzi Tanzania (TANNA) Mkoa wa Lindi, Patrick Achimpota (kulia) mwenyeshati la kitenge akisalimiana na mjumbe wa Kamati kuu ya Chama hicho kutoka Arusha, Hosea Naman mara alipofika Mkoani humo kwa niaba ya Mkutano Mkuu wa Chama hicho.


 Wajumbe wa Chama Cha Wauguzi (TANNA) wakiwa katika safari kuelekea Mkoa wa Lindi katika Mkutano Mkuu wa Chama hicho  unao tarajiwa kufanyika Oktoba 4-6 Kitaifa ambapo unatarajiwa kufunguliwa na Waziri Mkuu, Kasim Majaliwa.



 Muuguzi Mkuu wa Hospitali ya Mkoa Lindi, Damasiana Msala (kulia)  akizungumza na wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Chama Cha Wauguzi (TANNA) mara walipowasili katika mkoa huo jana
 Makamu wa Rais wa Chama hicho, Ibrahim Mgoo (wa katikati) akisalimia wajumbe mara baada ya kuwasili katika Mkoa huo jana, kulia ni Muuguzi Mkuu wa Hospitali ya Mkoa Lindi, Damasiana Msala na kushoto ni Katibu Mkuu wa Chama hicho, Sebastian Luziga. 

 
Supported by Tone multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Lindi Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa