Na Jacquiline Mrisho
Serikali
 imetenga jumla ya shilingi bilioni 48.3 kwa ajili ya kujenga Mahakama 
40 kwa mwaka wa fedha 2016/2017 ili kuongeza ufanisi na kuharakisha 
hukumu za kesi katika ngazi mbalimbali nchini.
Kutokana
 na fedha itakayotumika kujenga mahakama, shilingi bilioni 36 zinatokana
 na Bajeti ya mwaka huu wa fedha wakati shilingi bilioni 12.3 zilitolewa
 na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt John Pombe 
Magufuli.
Hayo
 yamebainishwa leo mjini Dodoma na Waziri wa Mambo ya Katiba na Sheria, 
Dkt. Harisson Mwakyembe alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Iramba 
Mashariki Mhe. Allan Kiula aliyetaka kufahamu ni lini Serikali itatoa 
fedha kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama za Wilaya na uteuzi wa Mahakimu 
katika ngazi hiyo.
Waziri
 Mwakyembe amesema kuwa Serikali imejipanga kuhakikisha Mahakama 
zinakuwepo kila wilaya ili kuwaondolea usumbufu wananchi, kurahisisha 
usikilizwaji wa kesi pamoja na kupunguza gharama kwa wananchi kutoka 
sehemu moja kwenda nyingine kufuata Mahakama zilipo.
“Kwa
 mujibu wa Katiba ya Nchi, Sheria na Kanuni inaeleza kuwa kila Mahakama 
ina mipaka yake hivyo hatuwezi kubadilisha mahakama ya mwanzo kutumika 
kama ya wilaya” amesema Dkt. Mwakyembe.
Ameongeza
 kuwa mpaka sasa bado kuna wilaya zinapata huduma ya Mahakama kupitia 
wilaya nyingine ambapo amewahakikishia Wabunge na wananchi kuwa Serikali
 itajenga mahakama 40 kwa mwaka huu wa fedha. 
Akifafanua
 mgawanyiko wa Mahakama 40 zinazotarajiwa kujengwa nchini, Dkt. 
Mwakyembe amesema kuwa Serikali itajenga Mahakama Kuu nne, Mahakama za 
mikoa sita, Mahakama za Wilaya 14 na Mahakama za Mwanzo 16 katika wilaya
 mbalimbali nchini.
Aidha,
 Mhe. Mwakyembe ametaja baadhi ya vigezo vinavyotumika kuanzisha 
Mahakama katika eneo lolote kuwa pamoja na uwepo wa hati ya kisheria ya 
kuwepo kwa wilaya, mkoa, kata na kijiji, umbali wa upatikanaji wa huduma
 za Mahakama, idadi ya wakazi wa eneo husika pamoja na uwepo wa huduma  zingine za kipolisi na magereza. 
Ameongeza
 kuwa kutokana na changamoto hizo za kukosekana kwa mahakama katika 
maeneo ambayo yamekidhi vigezo ndiyo yaliyopelekea Serikali kujipanga 
kujenga Mahakama hizo ambapo ametoa rai kwa wananchi kuwa na subira 
wakati wakikusubiri kujengwa kwa Mahakama hizo. 
MWISHO
 

 
 
 
 
0 comments:
Post a Comment