Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Mwenyekiti wa Taifa wa CUF, Prof. Ibrahim Lipumba.
Chama cha Wananchi (CUF) kimebaini kuwapo dosari 
lukuki katika uandikishaji wapigakura katika Daftari la Kudumu la 
Wapigakura unaondelea katika mikoa ya kusini ya Lindi, Mtwara na Ruvuma.
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, 
Mwenyekiti wa Taifa wa CUF, Prof. Ibrahim Lipumba, alisema viongozi wa 
CUF walifanya ziara katika mikoa hiyo na kukuta changamoto mbalimbali 
zikiwamo waandishi kutokuwa na uzoefu na mashine za BVR kutofanya kazi, 
hali iliyosababisha wananchi wengi kukosa haki zao za msingi.
“Katika vituo vingi, uandikishaji ulisuasua kwa sababu waandishi 
wengi walionekana kukosa uzoefu, mashine kushindwa kufanya kazi 
inavyotakiwa,” alisema na kuongeza: 
“Hali hii ilisababisha wananchi kuachwa bila kuandikishwa. katika daftari la wapigakura.”
Prof. Lipumba alisema walibaini kuwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi(Nec)
 haikufanya jitihada za kuhamasisha wananchi kujitokeza kwa wingi 
kushiriki kujiandikisha huku akisisitiza taarifa zilichelewa kufikishwa 
kwa wakati.
Aidha, alisema muda wa siku saba uliotengwa na Nec haukutosha 
kuandikisha wananchi wote wenye haki ya kuwa wapigakura akiiomba Nec 
iongeze angalau wiki mbili.
Alisema bajeti iliyotengwa kwa ajili ya kuandikisha wapigakura 
haitoshelezi kuweka waandishi wengi katika vituo kwa kuwa kwenye vituo 
hivyo kuna waandishi wawili wanaofanya kazi kuanzia saa 2:00 asubuhi 
mpaka saa12:00 jioni hali inayosababisha kushindwa kuwahudumia wananchi 
ipasavyo.
Prof. Lipumba alisema katika baadhi ya wilaya kama Tunduru BVR kits
 hazitumiwi kutokana na Nec kutokuwa na fedha za kutosha za kuwalipa 
waandikishaji huku akitaja waandishi hulipwa Sh. 100,000 kwa wiki wengi 
wao wakiwa wanakaa katika maeneo ambayo siyo nyumbani.
Aliongeza kuwa baadhi ya  vituo kulikuwa na matatizo ya 
kutotambuliwa kituo ambacho mpiga kura amejiandikisha na kitambulisho 
alichopewa akitolea mfano wilaya ya Newala kituo cha kuandikisha cha 
Mahoha, kadi ya mpigakura ilisomeka Nambari A  wakati kijiji cha Nambali
 kiko kilometa 15 kutoka kituoni hapo.
Alisema katika Kata ya Michemo kituo cha kuandikisha cha Mchemo A 
kadi ya mpiga kura ilisomeka kata ya Mpwapwa huku waandikishaji 
waliondolewa wakiwa wameandikisha watu 31 wakati makadirio ya kata nzima
 ni wapiga kura 3059.
Alifafanua katika Wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma, Naibu Katibu 
Mkuu wa CUF Bara, Magdalena Sakaya, alishuhudia wananchi wengi ambao 
hawakuandikishwa katika vituo wiki ya kwanza, lakini mashine za BVR 
zilondolewa na kwamba alipomuuliza mkurugenzi wa wilaya hiyo hakuwa na 
majibu kwa wananchi.
Pia, katika kijiji cha Mlonde kata ya Mtemanga wilaya ya Tunduru, 
alisema asilimia 60 ya wananchi wenye haki ya kuwa wapigakura 
hawakuandikishwa na cha kushangaza mashine zilihamishwa.
Alisema idadi ya wapiga kura ni 2,260, lakini walioandikishwa ni 
920 tu huku katika Kata ya Namwinyu kiyuo cha Uliya na Ndenyenge siku 
mbili za mwanzo walaindikishwa watu wanne tu.
Prof. Lipumba alisema ugawaji wa BVR kit hauna uwiano na idadi ya 
wapiga kura waliopo kwenye vituo  akitolea mfano Kata ya Majimaji 
wilayani Tunduru, kituo cha shule ya msingi na Chalinze kina wapigakura 
8,000, lakini kila kituo kilipewa mashine moja.
Alisema kuna vituo vyenye wapigakura 200 mpaka 1,000 vimepewa BVR 
kit mbili hadi nne wakati vituo vyenye watu 2,000-2,800 vilipewa BVR 
kits moja.
Hata hivyo, Prof. Lipumba alisema  kuna mikakati ya kuonekana tume 
imefikia mikoa yote bila kuwapa fursa wananchi wote wenye haki ya kuwa 
wapigakura kujiandikisha akibainisha kuna hatari wengi wakanyimwa fursa 
ya kuwa wapigakura.
Aliitaka serikali iipe Nec fedha za kutosha kukamilisha  mchakato 
wa kuandikisha na kuacha kupoteza fedha nyingi katika maandalizi ya kura
 ya maoni ya Katiba Inayopendekezwa.
Alipoulizwa Mwenyekiti wa Nec, Jaji Mstaafu Damian Lubuva, alisema 
mchakato wa uandikishaji unaendelea vizuri na dosari hizo zitatatuliwa 
daftari litakapokamilika kwa kuangalia maeneo husika.
“Niko mkoani Mtwara wilayani Masasi, uandikishaji unaendelea vizuri
 hakuna dosari kubwa ni ndogo ndogo ambazo haziwezi kuathiri, 
zitarekebishwa mara tu daftari likapokamilika, alisema Jaji Lubuva.
Alisema katika maeneo ambayo mashine za BVR zilionekana 
kutokutosheleza idadi ya wapiga kura zilichukuliwa sehemu nyingine na 
kupelekwa katika maeneo hayo.
     CHANZO:
     NIPASHE
    
 
 
 
 
 
0 comments:
Post a Comment