Home » » MAMA KIKWETE AWATAKA VIJANA KUWA WAZALENDO NA KUTOKUBAGUANA BALI WASAMBAZE UPENDO‏

MAMA KIKWETE AWATAKA VIJANA KUWA WAZALENDO NA KUTOKUBAGUANA BALI WASAMBAZE UPENDO‏

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Mke wa Rais Mama Salma Kikwete akitoa hotuba ya uzinduzi rasmi wa Klabu Zalendo iliyoko katika Halmashauri ya Manispaa ya Lindi kwenye Uwanja wa Ilulu tarehe 10.5.2015.  Aliyekaa kushoto kwa Mama Salma ni Mkuu wa Wilaya ya Lindi Bwana Yahaya Nawanda na kulia ni Mwenyekiti wa Klabu Zalendo Mwalimu Mwajuma Malugu.  
PICHA NA JOHN LUKUWI. 


Na Anna Nkinda – Lindi
Vijana mkoani Lindi wametakiwa kuwa wazalendo na kutobaguana bali wasambaze upendo na kujiona wote ni sawa kwa kufanya hivyo wataondoa chuki na kudumisha amani, mshikamano na umoja katika jamii inayowazunguka.
Mwito huo umetolewa na Mke wa Rais Mama Salma Kikwete wakati akifungua klabu zalendo zilizopo katika  Manispaa ya Lindi.
Mama Kikwete ambaye ni Mke wa Rais Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete alisema kama jamii itajenga tabia ya ubaguzi italeta chuki na upendo utatoweka na hivyo kusababisha vurugu zitakazopoteza  amani iliyopo.
Alisema uzalendo ni kiini cha maendeleo hivyo huwezi kuwa mzalendo kama hupingi rushwa na matumizi ya madawa ya kulevya, hutunzi mazingira, hushiriki kuchangia utoaji wa damu salama na kutokuchangamkia fursa mbalimbali za maendeleo zilizopo katika jamii yako.
Mama Kikwete alisema, “Leo hii nimezindua klabu zalendo, Mzalendo ni mtu mwenye huruma na mtu anayeona thamani ya kitu alichonacho tunzeni vitu mlivyonavyo ikiwemo Amani ya nchi yetu na mjitoe kufanya kazi kwa bidii ili muweze kupata maendeleo.
Aidha Mama Kikwete  aliwahimiza wanafunzi kujitendea haki kwa kusoma kwa  bidii hadi elimu ya chuo kikuu kwa kufanya hivyo wataweza kuajiriwa na kujiajiri katika katika fani mbalimbali na kujiletea maendeleo katika mkoa wao wa Lindi.
Akisoma historia fupi ya klabu zalendo Mwalimu Mwajuma Malugu ambaye ni Mwenyekiti alisema lengo kuu la kuanzishwa kwa klabu hiyo ni kuutetea na kuulinda muungano wa Tanganyika na Zanzibari ndiyo maana wanatumia namba za #26464#ikimaanisha tarehe 26 mwezi wa 4 mwaka 1964 siku ya muungano. 
Aliyataja malengo mengine kuwa ni kuhamasisha wanafunzi na vijana waliopo mtaani kuwa wazalendo na kuipenda nchi yao kwa kufanya hivyo wataepukana na mambo yasiyofaa kwa maslai ya nchi yao.
“Mafanikio tuliyoyapata ni kujenga umoja na ushirikiano, kuongeza idadi ya wanachama na hii inatokana na kufunguliwa kwa matawi mengine ya uzalendo mashuleni na mitaani, kuongeza na kupanua uelewa kwa wanafunzi na raia kuhusu  klabu ya uzalendo, kuwahamasisha watu kuwa wazalendo na kujitoa katika uchangiaji wa damu, kupinga rushwa, madawa ya kulevya pamoja na kulinda Amani ya nchi.
Mwalimu Mwajuma alizitaja changamoto wanazokabiliana nazo kuwa ni uhaba wa fedha kwa ajili ya kuandaa makongamao na mabonanza yatakayosaidia  kuimarisha harakati zote za klabu ya uzalendo na kushindwa kutuma wawakilishi katika mikutano na makongamano ya wanaklabu ngazi ya taifa. 
Pia kikundi kimekosa semina kwa wanaklabu hali inayoplekea wanachama  kukosa uelewa wa kutosha kuhusu madhumuni ya klabu hiyo.
Klabu zalendo ilianzishwa na walimu wa Shule ya Sekondari Lindi katikati mwa mwaka jana hadi sasa inawanachama 1450 kutoka shule za Sekondari Mkonge, Angaza, Ngongo, Ng’apa, Chikonji, Mingoyo, Kineng’ene , chuo cha ufundi VETA na walimu wa shule za msingi pamoja na wanafunzi wao.
Pia klabu hiyo imehusisha vijana kutoka mtaani wanaofanya kazi za udereva wa pikipiki maarufu kama bodaboda, wavuvi na wanavikundi vya Sanaa.
Mama Kikwete aliahidi kukipatia kikundi hicho  mipira 20 na jezi seti 10 kwa ajili ya wanafunzi wa shule za msingi na Sekondari ambao watashiriki katika mashindano mbalimbali `na kuangalia utaratibu wa kuwapatia mradi ambao utawasaidia kuwainua kichumi.

0 comments:

 
Supported by Tone multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Lindi Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa