Home » » ZITTO: TUMECHEZEA ELIMU YETU TUTAJUTA

ZITTO: TUMECHEZEA ELIMU YETU TUTAJUTA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
  Mbunge huyo anayesifika kwa kujenga hoja bungeni, anahoji wanapokwenda nusu ya wanafunzi wanaomaliza shule kila mwaka na kushindwa kuendelea na masomo
Kila baada ya matokeo ya mitihani ya taifa kutolewa, taifa hugubikwa na mijadala mingi kuhusu hali ya elimu nchini.
Hata hivyo, mijadala hiyo hupita kama upepo, japo mara nyingi matokeo hayo huacha simanzi kubwa kuhusu hali halisi ya sekta ya elimu ilivyo nchini.
Ni simanzi itokanayo na matokeo mabaya ambayo pia yanaonyesha kuwepo kwa walakini katika sekta ya elimu.
Walakini huu kwa mujibu wa mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe haujatafutiwa mwarobaini na kibaya zaidi haoni jitihada zozote za dhati za kurekebisha hali ya mambo kabla hayajaharibika.
“Kwa jumla, sekta ya elimu imetelekezwa na watu wanazungumza kama elimu haina mwenyewe. Iko haja ya kuzungumza kwa umakini kabla mambo hayajaharibika kabisa,’’ anasema.
“Tunahitaji kuhakikisha kwamba kuna usimamizi mzuri katika elimu. Hivi sasa yanatoka matokeo mabaya kidato cha nne au sita watu wanapiga kelele, lakini baada ya wiki tunaendelea na maisha kama kawaida.”
Zitto, mbunge kijana aliyejizolea sifa kubwa katika duru za siasa nchini, anasema hali duni ya elimu inajidhihirisha katika shule za umma ambazo miaka ya nyuma zilikuwa kimbilio la wengi, lakini sasa zinakimbiwa.
Enzi hizo, anasema Zitto kuwa wazazi walifikia hatua ya kufanya hila na udanganyifu, alimradi watoto wao wasome katika shule hizo zilizokuwa zikitamba kwa taaluma.
Hali ya sasa ya elimu
Zito anataja masuala kadhaa yaliyosabaisha sekta ya elimu kuwa katika hali mbaya kuwa ni pamoja na uamuzi wa Serikali kuwaondoa wakaguzi wa elimu shuleni.
“Kuua wakaguzi wa elimu kumeshusha kiwango cha elimu. Nakumbuka wakati nasoma, mkaguzi alikuwa anaingia darasani anasimama nyuma, anamwangalia mwalimu wakati anafundisha. Hii ilichochea uimara wa elimu wakati ule,” anasema.

Suala jingine ni walimu na mchango katika kukuza kiwango cha elimu nchini.
Anasema taifa haliwezi kuzungumzia elimu bila kuwatazama walimu anaosema ni roho ya taifa katika kuandaa rasilimali ya taifa.
“Ndiyo maana wengine tunaona tukiachana na siasa tutakwenda kufundisha, kwa sababu ni kazi inayosaidia kuzalisha rasilimali watu,” anaeleza.
Hata hivyo, anasema badala ya kujali wajibu huu walio nao walimu, watumishi hao wamekuwa wakifanya kazi katika mazingira yanayosikitisha, hivyo kuathiri maisha na ustawi wao.
“Tutapata pesa za rada tutanunua vitabu, zitakuja nyingine zitanunua madawati, lakini kama maisha ya walimu wetu hayataboreshwa ni nani atakayewaelimisha watoto? “ anahoji.
Kwa kuwa anaamini walimu ndiyo nguzo ya elimu, anasema aliwahi kushauri walimu hasa wanaofundisha maeneo ya vijijini kulipwa mara mbili ya mishahara ya kawaida.
“Niliwahi kutoa wazo kuwa kwa nini elimu isiwe na mfumo wake peke yake. Niliwahi kuwahoji wenzangu kwa nini tusiwape walimu wa vijijini mshahara mara mbili ya kawaida ili kuwavutia kuendelea kubaki, lakini wenzangu wakasema ‘aah sijui nini na nini’. Nikawaambia elimu siyo majengo, bali ni hawa wenzetu wanaofundisha,” anasema.
Walimu kunyonywa
Zitto anasema pamoja na walimu kuwa katika hali ngumu, bado wanaandamwa na madeni mengi kutoka katika taasisi za fedha nchini zinazowatoza riba kubwa.
“Jimboni kwangu kuna tatizo kubwa la walimu na mikopo, naamini hili lipo nchi nzima kwa sababu nimeshawahi kulisikia, yaani, mwisho wa mwezi mwalimu mshahara wake ni sifuri,’’ anasema.
“Niliongea na Mukoba (Gratian), wakati ule akiwa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), huyu ambaye sasa yupo Tucta, nikamuuliza kwa nini chama chenu kisiwe na benki yake wenyewe ili imkopeshe kwa riba ndogo?
“Nikamwambia hivi nyinyi mnakusanya fedha za walimu, PSPF (Mfuko) wa Pensheni kwa Watumishi wa Umma wanakusanya fedha za walimu.
Asilimia 60 ya wachangiaji wa mfuko huo ni walimu, nikamwambia lazima CWT na PSPF wakutane waone jinsi wanavyoweza kuwasaidia wateja wao (walimu) katika kukabiliana na janga la mikopo. Kwenye vikundi wanawatoza mpaka riba za asilimia 40.
Swali la kujiuliza
Mbunge huyo anayesifika kwa kujenga hoja bungeni, anahoji wanapokwenda nusu ya wanafunzi wanaomaliza shule kila mwaka na kushindwa kuendelea na masomo.
“Asilimia 50 ya watoto wanafeli mitihani, wanakwenda wapi? Hapa tunapozungumza watoto milioni 12 wapo shuleni, yaani msingi na sekondari. Tujiulize, wanakwenda wapi baada ya hapa?” anahoji.
Ili kujinusuru na hili, anashauri serikali na wadau kuwekeza ipasavyo katika mfumo wa elimu ya ufundi kama njia ya kuwasaidia wanafunzi hao wanaoshia njiani.
“ Hiki kitu hakitakuwa kipya, kulikuwa na shule za ufundi za Dar Tech, Mbeya, Moshi, Tanga na nyinginezo. Waanzilishi wa taifa hili walikuwa na maono kwamba si kila mtu tunaweza kumpeleka chuo kikuu,” anaeleza.
Anakumbushia ahadi ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ya kujenga chuo cha ufundi kila wilaya na kwamba hata sasa inawezekana kufanya mabadiliko kwa kuzijenga nyingine kwa kuzitumia kambi za mafunzo ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT).
“Kila kambi ya JKT iwe ni chuo cha ufundi, unahitaji Sh796 bilioni ili kuwa na chuo kila wilaya. Fedha hizi huwezi kuzipata mara moja, ila unachoweza kufanya ni kuiunganisha Veta (Mamlaka ya Elimu ya Ufundi) na JKT,”anafafanua.
Anasema kuwa faida ya mfumo huu ni kuwa kila kijana anayehitimu atakuwa na uhakika wa kujiajiri na baadaye anaunganishwa na mifuko ya hifadhi ya jamii kwa manufaa ya baadaye.
“Kama ni seremala anapewa vifaa, yaani anatoka anakwenda moja kwa moja kujiajiri. Pia, hiyo mifuko ya jamii inakuwa imepata wanachama wa uhakika,” anasema na kuongeza:
“ Hivi sasa kuna kiwango cha hali ya juu cha uhalifu, hii yote inatokana na ukweli kwamba vijana wengi hawana kazi. Kila siku tunasikia watu wanapigwa risasi, kama hatutalifanyia kazi hii, ipo siku tutaamka, watu wa Manzese watavamia Masaki na kwa kuwa wanajua hawana cha kupoteza.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Lindi Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa