Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Natumaini wajukuu zangu ni wazima wa afya, mkiwa bado baadhi
yenu mnaendelea na mfungo wa Ramadhan. Leo wajukuu zangu nina mada
nyepesi ambayo naamini inawagusa wengi.Kabla ya kuanza mada yetu ya leo
ni vizuri tukafahamu maana ya uvivu.
Uvivu ni neno ambalo limezoeleka katika vinywa vyetu, lakini naamini wengi wenu hamfahamu maana ya neno hili.
Uvivu ni ile hali ya kutotaka kufanya kazi. Ukihisi una tabia ya kutotaka kufanya kazi bila shaka wewe ni mvivu.
Wapo baadhi ya watoto wanaamini eti, uvivu ni
ugonjwa ambao mtu anaweza kutibiwa hospitali. La hasha hilo si kweli.
Uvivu ni tabia tu ambayo mtu anajizoesha na baadaye anajikuta linakuwa
jambo la kawaida kwake.
Baadhi ya watoto huwa wanaanza tabia ya uvivu kwa
kukwepa kufanya kazi za nyumbani na kama mzazi hajagundua hilo mapema
mtoto huyo ataendelea na tabia hiyo hata katika masomo yake darasani.
Mwanafunzi mwenye tabia ya uvivu hatoweza kufanya
mazoezi aliyoagizwa na mwalimu na hasara ya kwanza atakayoipata ni
kushindwa kujipima katika mitihani kwa kile alichosoma na hatimaye
lazima atafeli mitihani yake.
Pia inaweza kupeleka mwanafunzi mwenye tabia hiyo
ya uvivu kuwa mtoto au kuacha kabisa shule kwa sababu hapendi
kubughudhiwa kama hajaandika au kukwepa kufanya mazoezi darasani.
Mtoto mwenye tabia ya uvivu kama hatokemewa na
kuacha tabia hiyo anaweza kuwa mvivu hata katika mambo ya msingi katika
maisha yake ya kila siku. Mfano anaweza kuwepa kuchota maji yake ya
kuoga sababu tu ya uvivu umemtawala na matokeo yake anapata magonjwa ya
ngozi kwa kukosa kuoga.
Ni vyema wazazi mkahakikisha watoto wenu wasiwe na
tabia ya uvivu ili waweze kujiepusha na madhara kama hayo. Ni vizuri
wazazi wakajenga tabia ya kuhakikisha watoto wanashiriki kazi za
nyumbani ipasavyo na kushirikiana kwa karibu na walimu ili kujua tabia
za watoto wenu kama kuna tatizo muweze kulitatua mapema.
Pia wazazi mnatakiwa kuhakikisha watoto wanafanya
mazoezi ya viungo ni njia nzuri ya kumfanya mtoto aondokane na uvivu.
Mazoezi yatawasaidia pia wawe na afya bora na kuwa wakakamavu na
wachapakazi wazuri. Nina imani wajukuu zangu wote mliokuwa na tabia ya
uvivu mtaiacha tabia hiyo na mtaanza mazoezi ili msiwe wavivu tena
Chanzo:Mwananchi
0 comments:
Post a Comment