Home » » MIFUKO YA JAMII YAOMBWA KUTATUA KERO ZA WANACHAMA VIJIJINI

MIFUKO YA JAMII YAOMBWA KUTATUA KERO ZA WANACHAMA VIJIJINI

Serikali imeitaka mamlaka ya usimamizi wa sekta ya hifadhi za jamii SSRA kujenga utamaduni wa kuhimiza mifuko ya hifadhi za jamii kutembelea mikoani ili kutatua kero za wanachama ikiwa ni pamoja na kujitangaza ili kuhamasisha wafanyakazi wa serikali na mashirika ya umma kujiunga na mifuko hiyo.
Hayo yamesemwa na mkuu wa mkoa wa Lindi Ludovick Mwananzila wakati akifunga warsha ya mafunzo ya kutoa elimu kuhusiana na sekta ya hifadhi ya jamii kwa viongozi wa mkoa wa Lindi ambapo amesisitiza juu ya wananchi kujiunga na mifuko ya namna hiyo.
Amewataka waajiriwa wote wa serikalini na katika mashirika ya umma kuwa na tabia ya kutunza kumbukumbu zao za ajira ili kupunguza adha ambazo huweza kutokea mara baada ya kufikia ukomo katika ajira na kusababisha kucheleweshwa kupata mafao yake.
Afisa TAKUKURU mkoa wa Lindi Steven Chami akitoa hoja katika mafunzo hayo ameiomba mamlaka hiyo kutoishia kuelimisha viongozi wa ngazi za juu pekee na badala yake itafutwe namna ya kuelimisha watu wengi zaidi ili kupunguza manung’uniko kwa wanachama kwa kuingizwa katika mifuko  hawaifahamu wala  kujua manufaa watakayopata kutokana na mfuko huo.
Naye mkuu wa mawasiliano na uhamasishaji wa SSRA Sarah Kibonde Msika amesema kuwa dhima ya mamlaka hiyo ni kuhakikisha wanachama wa mifuko ya hifadhi za jamii wanapatiwa huduma zilizo bora bila ya kujali kazi au kipato chake.
Mpaka sasa Tanzania bara kuna mifuko mitano ya hifadhi ya jamii na Tanzania visiwani mfuko mmoja ambapo takwimu zinaonesha kuwa wanachama zaidi ya milioni moja na nusu wananufaika na mifuko hiyo.

0 comments:

 
Supported by Tone multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Lindi Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa