| 
      KITUO  cha Uwekezaji Tanzania (TIC) kimetakiwa kufuatilia wawekezaji wote ili kuona  kama mikataba waliyoingia inafuatwa.Kauli  hiyo ilitolewa bungeni jana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri 
Mkuu, Uwekezaji  na Uwezeshaji, Dk. Mary Nagu, alipokuwa akijibu swali 
la nyongeza la Mbunge wa  Kilwa Kaskazini, Murtaza Mangungu (CCM).
 Katika  swali lake, mbunge huyo alisema hivi sasa kuna wawekezaji 
kutoka China,  Marekani na Hong Kong na imefikia hatua wameingia kwenye 
biashara ya uuzaji wa  bidhaa ikiwa ni pamoja na kufungua maduka.
 Alitaka  kujua ni uwekezaji wa aina gani unaofanyika na ni lini uhakiki wa wageni hao utafanywa.
 Akijibu  swali hilo, Dk. Nagu alisema kufanya biashara si uwekezaji 
ila uwekezaji ni  kwenye kilimo, viwanda na maeneo mengine ya 
uzalishaji.
 Alisema  uwekezaji wowote lazima ulete masilahi kwenye nchi ambayo inapokea wawekezaji.
 Katika  swali la msingi, mbunge huyo alitaka kujua ni sababu zipi 
zinazochangia raia wa  kigeni kuzagaa hovyo katika maeneo ya vijijini na
 kushindania fursa kibiashara  na wazawa.
 Pia,  alihoji kwa nini serikali isiamuru raia hao kubaki katika maeneo ya miji mikuu  pekee.
 Akijibu  swali hilo kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, 
Naibu Waziri wa  Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Amos Makalla, 
alimuomba mbunge na  wananchi kwa ujumla kutoa taarifa za raia yeyote wa
 kigeni anayezagaa nchini  bila kibali kwa Kamati ya Ulinzi na Usalama, 
ili hatua stahiki za kisheria  zichukuliwe dhidi yao.
 CHANZO;MWANANCHI
 
 | 
0 comments:
Post a Comment