Home » » Bima ya afya yaonya watoa huduma

Bima ya afya yaonya watoa huduma



MFUKO wa Taifa wa Bima ya Afya imetoa onyo kwa watoa huduma ambao si waaminifu kuwa itawachukulia hatua kali ikiwemo kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria  kwani kuna wanaojihusisha na kugushi hati na kujipatia malipo kwa njia ya udanganyifu. Onyo hilo limetolewa juzi na Mjumbe wa Bodi  ya Wakurugenzi  ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya, Charles Kajege, kwenye mkutano wa Kongamano la  wadau wa Mfuko wa Taifa wa  Bima ya Afya na Mfuko wa Afya ya Jamii uliofanyika  kwenye ukumbi wa Kagwa  mjini Lindi.
Alibainisha kuwa kuna baadhi ya wahudumu wamekuwa wadanganyifu kwa lengo la kujipatia fedha  kwa kujaza taarifa za uongo.
Katika kukabiliana na changamoto hiyo, Kajege alisema kuwa bodi imeanza kuchukua hatua mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuuagiza uongozi wa mfuko  kuwasilisha mapendekezo  ya namna  ya  kulitatua  ikiwa ni pamoja na kuliwekea sera yake na namna ya kulishughulikia.
Mjumbe huyo alitaja changamoto nyingine kuwa ni baadhi ya wanachama  kutumia kitambulisho kimoja kwa  watu wengine ambao si wanachama wa mfuko   na kuwa wamejipanga kuhahakikisha kuwa wanachama wanaostahili tu ndio wanaopata huduma na katika kuhakikisha hilo na katika kudhitibi hilo mfuko umeamua kila  hospitali kubwa inakuwa na maafisa wa mfuko wa taifa wa Bima ya Afya  kwa ajili ya udhibiti na ufuatiliaji zaidi.
“Tunachukua hatua za kushirikisha vyombo vingine vya dola na mamlaka nyingine za kisheria na serikali katika suala hili ikiwemo kuwapeleka katika vyombo vya sheria wahusika wote punde wanapobainika,” alisema Kajege.
Kwa upande wake Mkuu wa mkoa wa Lindi, Ludovick Mwananzila, ambaye alikuwa mgeni rasmi, aliwataka viongozi  wote wa mkoa huo  kuhakikisha  wanaongeza kasi ya uhamasishaji kwa jamii ili wajiunge kwenye  mifuko hiyo.
Alisema kwa sasa mkoa una wanachama wanaonufaika na huduma za mfuko wa afya ya jamii (CHF), Kaya 225,972.

Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Lindi Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa