Home » » Kilwa wahimizwa kujiunga CHF

Kilwa wahimizwa kujiunga CHF


WANANCHI wa Kilwa Masoko, mkoani Lindi, wameshauriwa kujiunga na Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF), ili waweze kutibiwa kirahisi pale wanapopatwa na maradhi mbalimbali.
Ushauri huo ulitolewa juzi na Mkuu wa Wilaya ya Kilwa, Abdalah Ulega, kwenye hotuba yake iliyosomwa na  Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa, Ado Mapunda, wakati wa uzinduzi wa kampeni ya kuhamasisha shughuli za CHF.
Alisema mfuko huo ni msaada na mkombozi wa kweli wa afya za jamii, lakini wananchi wengi bado hawajaelewa faida na manufaa yake.
“Nimetaarifiwa wananchi wanaoufaidika na huduma za mfuko huu hadi Juni 30, mwaka huu hapa Kilwa ilikuwa ni kaya 365 wakati wenzetu wa Liwale waliojiunga ni kaya 9,137. Jitihada za makusudi lazima zifanyike sasa ili kuibadilisha Kilwa,” alisema.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya ya Jamii, Hamisi Mdee, alisema jumla ya halmashauri 120 zinatekeleza huduma za CHF na kaya zinazochangia ni 543,621 sawa na wanufaika milioni 3.2 ambayo ni asilimia 7.5 ya walengwa.
“Uandikishaji wa wanachama wa CHF katika daftari maalumu kwa ajili ya kuwapatia namba za huduma za uanachama wa CHF nchi nzima tayari limekwishaanza katika halmashauri 10 kabla ya kufanyika nchi nzima…tunaomba wadau wetu watupe ushirikiano ili kuboresha kumbukumbu na taarifa hizo,” alisema.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Lindi Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa