Home » » Tume ya Mipango yashauri Sekta Binafsi Kuchangamkia Fursa za Mikopo

Tume ya Mipango yashauri Sekta Binafsi Kuchangamkia Fursa za Mikopo

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 



Na Adili Mhina, Lindi
Tume ya Mipango imefanya ziara katika mradi wa ufugaji ngo’ombe na uzalishaji wa maziwa unaoendeshwa na watawa eneo la Narunyu wilayani Lindi na kushauri uongozi wa mradi huo kutumia fursa za mikopo ya kilimo ili kupanua wigo wa uzalishaji wa mazao ya mifugo pamoja na kuongeza uzalishaji wa nishati ya umeme kwa kutumia kinyesi cha wanyama.

Mradi huo umekuwa ukizalisha maziwa na nyama kwa ajili ya biashara huku nishati ya umeme kwa ajili kuendesha shughuli za kiwanda hicho ikiwa inazalishwa kutokana na kinyesi cha wanayama hao.

Kwa sasa uzalishaji umepungua baada ya kiwanda kushindwa kuzalisha nishati ya umeme ya kutosha na kuanza kutegemea umeme wa tanesco ambao kwa mujibu wa mmoja wa wasimamizi wa mradi huo, Bi Yasinta Mrose umesababisha gharama za uzalishaji kuongezeka.

Changamoto nyingine ni  kuharibika kwa baadhi mashine zinazotumika kuandaa malisho ya ngo’ombe, ukosefu wa soko la karibu kwa mazao ya nyama na maziwa, pamoja na uhaba wa maeneo kwa ajili ya malisho ambapo kwa sasa mradi una zaidi ya ng’ombe 400.

Kutokana na changamoto hizo, Kaimu Katibu Mtendaji Tume ya Mipango Bibi Florence Mwanri aliueleza uongozi huo kuwa ni vyema wafanye taratibu za kuomba mkopo hususani katika benki ya kilimo ili waweze kuongeza mtaji, uzalishaji na kupanua soko.

“Huu ni mradi mzuri na msirudi nyuma katika uzalishaji wenu, nawashauri mkae mjadiliane muone namna ya kupata mkopo ili muweze kununua mashine za kisasa na muongeze uzalishaji. Bila kuchukua hatua hizo mnaweza mkashangaa mradi unakufa wakati unafaida kwenu na hata kwa wananchi wanaowazunguka,” alieleza.

Kuhusu changamoto ya soko la karibu, Mwanri alieleza kuwa uongozi unapaswa kufikiria kuzalisha maziwa na kutengeneza bidhaa zinazotokana na maziwa na kusafirisha nje ya wilaya ya Lindi kwani soko bado ni kubwa.

Aliongeza kuwa hatua iliyofikiwa ya kuzalisha umeme wa kutosha kuhudumia shughuli zote za uzalishaji kiwandani hapo ni nzuri na Serikali inaiunga mkono jitihada za sekta binafsi katika kukuza maendeleo ya uchumi ikiwa ni njia ya kutekeleza malengo ya Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2016/17-2020/21).

“Nimefarijika sana kusikia mlikuwa mnazalisha umeme wa kuwatosheleza, mmejitahidi kutekeleza mpango wa Taifa wa Maendeleo kwa vitendo. Tume ya Mipango inatambua na kuunga mkono jitihada zenu hivyo nawasihi shirikianeni na Halmashauri kufanya kila linalowezekana ili shughuli zenu ziendelee zaidi ya mlivyokuwa mnazalisha huko nyuma,” aliongeza.

0 comments:

 
Supported by Tone multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Lindi Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa