Home » » Watumishi 2,500 kukopeshwa kuku

Watumishi 2,500 kukopeshwa kuku

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 


MKUU wa Wilaya ya Lindi, Yahaya Nawanda ameandaa utaratibu wa kuwakopesha kuku watumishi wote zaidi ya 2,500 wa Halmashauri ya wilaya hiyo na Manispaa kwa ajili ya kujiongezea kipato na kuboresha afya zao na ameagiza kila mtumishi kutekeleza hilo.
Utaratibu huo unaanza kutekelezwa mwishoni mwa mwezi huu kwa makubaliano baina ya Mkuu huyo wa Wilaya na wakurugenzi watendaji wa halmashauri na manispaa ambao mwishoni mwa mwezi huu wataanza na wakuu wote wa Idara na mapema Julai watachukua watumishi wengine.
Akizungumza na gazeti hili juzi, alisema wameanzisha mradi wa kuku wilayani humo kwa ajili ya kuviwezesha vikundi, wanawake, vijana na watumishi wa serikali kujiongezea kipato na wamekubaliana kila mkuu wa idara achukue kuku wasiopungua 30 mwisho wa mwezi huu.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Lindi, Jomaary Satura, halmashauri hiyo ina watumishi 1,741. Mkuu wa Wilaya alisema kwa upande wa Manispaa kuna watumishi 950 na watapaswa kuchukua kuku na kurejesha fedha kwa awamu kwa kipindi cha miezi sita.
“Hii ni amri halali, si hiari, hatutaki kuona mtumishi akilalamika hali ngumu ya maisha, hii falsafa ya mkuu wa nchi, Rais John Magufuli ya Hapa Kazi Tu ni kwa wote, hivyo nimeamua kuwakopesha kuku watumishi wote wa Lindi,” alisisitiza Nawanda.
Akifafanua zaidi, alisema wana mradi wa kuku zaidi ya 50,000 na watumishi wa Lindi watachukua kuku pamoja na viuatilifu zikiwamo dawa na atakuwa na hiari ama ya kuwala kuku wote ama kufuga na baadaye kuuza mayai na mengine kula kuimarisha afya zao.
“Kwa mfano, kuku mmoja anauzwa kwa shilingi elfu tatu, akichukua kuku 30 ni shilingi elfu tisini, akilipa kwa miezi sita kila mwezi itakuwa ni shilingi 15,000. Akiamua kula wote sawa, akifunga kwa tija apate mayai, vifaranga na kuuza pia sawa,” alisema.
Alipoulizwa haoni kama ni kumlazimisha mtu kufanya jambo asilolitaka ikiwa itakuwa amri kwa wote, alisema ndio maana wameweka uhuru kwa mhusika akitaka kuchinja kuku wote ni sawa ilimradi asije kusema hakuwezeshwa.
Alisema anataka wakuu hao wa idara na watumishi kuwa mfano katika mradi wa ufugaji kuku ili kusaidia kuielimisha jamii inayowazunguka faida na umuhimu wa ufugaji huo kwa uchumi wa mtu mmoja na Taifa kwa ujumla.
Mmoja wa wakuu wa idara katika halmashauri hiyo, Mkuu wa Idara ya Mipango Miji na Maliasili, Michael Mlyambongo, alisema yeye atachukua kuku 100 na matarajio yake ni kufikisha kuku 500 ili kujiongezea kipato. Meneja wa Mradi wa Kuku, Salma Zahoro alisema wanajitahidi kuinua vipato vya Watanzania.
Chanzo Gazei la Habari Leo
 

0 comments:

 
Supported by Tone multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Lindi Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa