MKUU wa Wilaya ya Lindi, Yahaya Nawanda ameandaa utaratibu wa 
kuwakopesha kuku watumishi wote zaidi ya 2,500 wa Halmashauri ya wilaya 
hiyo na Manispaa kwa ajili ya kujiongezea kipato na kuboresha afya zao 
na ameagiza kila mtumishi kutekeleza hilo.
Utaratibu huo unaanza kutekelezwa mwishoni mwa mwezi huu kwa 
makubaliano baina ya Mkuu huyo wa Wilaya na wakurugenzi watendaji wa 
halmashauri na manispaa ambao mwishoni mwa mwezi huu wataanza na wakuu 
wote wa Idara na mapema Julai watachukua watumishi wengine.
Akizungumza na gazeti hili juzi, alisema wameanzisha mradi wa kuku 
wilayani humo kwa ajili ya kuviwezesha vikundi, wanawake, vijana na 
watumishi wa serikali kujiongezea kipato na wamekubaliana kila mkuu wa 
idara achukue kuku wasiopungua 30 mwisho wa mwezi huu.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Lindi, Jomaary 
Satura, halmashauri hiyo ina watumishi 1,741. Mkuu wa Wilaya alisema kwa
 upande wa Manispaa kuna watumishi 950 na watapaswa kuchukua kuku na 
kurejesha fedha kwa awamu kwa kipindi cha miezi sita.
“Hii ni amri halali, si hiari, hatutaki kuona mtumishi akilalamika 
hali ngumu ya maisha, hii falsafa ya mkuu wa nchi, Rais John Magufuli ya
 Hapa Kazi Tu ni kwa wote, hivyo nimeamua kuwakopesha kuku watumishi 
wote wa Lindi,” alisisitiza Nawanda.
Akifafanua zaidi, alisema wana mradi wa kuku zaidi ya 50,000 na 
watumishi wa Lindi watachukua kuku pamoja na viuatilifu zikiwamo dawa na
 atakuwa na hiari ama ya kuwala kuku wote ama kufuga na baadaye kuuza 
mayai na mengine kula kuimarisha afya zao.
“Kwa mfano, kuku mmoja anauzwa kwa shilingi elfu tatu, akichukua kuku
 30 ni shilingi elfu tisini, akilipa kwa miezi sita kila mwezi itakuwa 
ni shilingi 15,000. Akiamua kula wote sawa, akifunga kwa tija apate 
mayai, vifaranga na kuuza pia sawa,” alisema.
Alipoulizwa haoni kama ni kumlazimisha mtu kufanya jambo asilolitaka 
ikiwa itakuwa amri kwa wote, alisema ndio maana wameweka uhuru kwa 
mhusika akitaka kuchinja kuku wote ni sawa ilimradi asije kusema 
hakuwezeshwa.
Alisema anataka wakuu hao wa idara na watumishi kuwa mfano katika 
mradi wa ufugaji kuku ili kusaidia kuielimisha jamii inayowazunguka 
faida na umuhimu wa ufugaji huo kwa uchumi wa mtu mmoja na Taifa kwa 
ujumla.
Mmoja wa wakuu wa idara katika halmashauri hiyo, Mkuu wa Idara ya 
Mipango Miji na Maliasili, Michael Mlyambongo, alisema yeye atachukua 
kuku 100 na matarajio yake ni kufikisha kuku 500 ili kujiongezea kipato.
 Meneja wa Mradi wa Kuku, Salma Zahoro alisema wanajitahidi kuinua 
vipato vya Watanzania.
Chanzo Gazei la Habari Leo
 
 

 
 
 
 
0 comments:
Post a Comment