Home » » JIEPUSHENI NA MAZINGIRA YATAKAYOWAPELEKEA KUPATA MIMBA ZA UTOTONI - MAMA SALMA KIKWETE

JIEPUSHENI NA MAZINGIRA YATAKAYOWAPELEKEA KUPATA MIMBA ZA UTOTONI - MAMA SALMA KIKWETE


Na Anna Nkinda – Maelezo, Masasi
Wanafunzi wa kike wilayani Masasi wametakiwa kuachana na tamaa za maisha zinazowapelekea kujiingiza katika mapenzi kabla ya wakati na hivyo kupata ujauzito unaowasababisha kukatiza masomo yao.

Ushauri huo umetolewa jana na Mke wa Rais Mama Salma Kikwete wakati akiongea na wananchi wakiwemo wanafunzi waliohudhuria hafla  ya makabidhiano ya gari la wagonjwa la Hospitali ya Mkomaindo iliyofanyika katika viwanja vya ofisi ya Mkuu wa wilaya hiyo.

Mama Kikwete ambaye ni Mwenyekiti wa Taasisi ya Wanawake na Maendeleo (WAMA) alisema kuna baadhi ya wanafunzi wanapenda maisha mazuri wakati wazazi wao hawana uwezo na hivyo kujiingiza katika mapenzi ili wapate fedha zitakazowafanya wanunue vitu wanavyohitaji.

“Wengine mnadiriki kufanya  mapenzi na watu wazima waliowazidi umri msifanye haya mambo kabla ya wakati. Ridhikeni na maisha ya wazazi wenu matokeo yake mtapata mimba na maambukizi ya Virusi Vya Ukimwi (VVU).

“Nawasihi wanangu msiruhusu mazingira ya kupata mimba mkiwa shuleni bali someni kwa bidii  na kufanya vizuri katika masomo yenu kwa kufanya hivyo mtakuwa na maisha mazuri hapo baadaye. Wavulana walindeni  dada zenu ili wasidanganywe na wanaume, nanyi pia someni muache tabia ya utoro hii itasaidia kuwa na Masasi ya wasomi”, alisisitiza Mama Kikwete.

Kwa mujibu wa  Taarifa ya Maendeleo ya Wilaya ya Masasi bado kuna tatizo kubwa la  wanafunzi wa kike kuacha shule kutokana na ujauzito. Mwaka 2013 wanafunzi 35 walipata ujauzito na mwaka  2014 waliopata ujauzito ni 22 na hivyo kukatiza masomo yao.

Akisoma taarifa hiyo Mkuu wa wilaya ya Nanyumbu ambaye ni Kaimu Mkuu wa wilaya ya Masasi Sauda Mtondoo alisema kupungua kwa idadi ya wanafunzi wanaopata ujauzito ni kutokana na kuanzishwa kwa vilabu vya wapinga mimba mashuleni na watuhumiwa wote wa tukio hilo kufikishwa mahakamani na kesi zao zinaendelea.

“Changamoto tunazokutana nazo ni walezi kutotoa ushirikiano kwa vyombo vya sheria pindi watoto wao wanapopata ujauzito, kesi nyingi zinamalizwa kinyemela, watuhumiwa kutoweka pindi wanapohusishwa na ujauzito wa mwanafunzi husika”, alisema Mtondoo.

Mkuu wa wilaya huyo aliitaja mikakati waliyonayo ni kutoa elimu kwa watoto ili wazielewe stadi za maisha, kuimarisha kitengo cha ushauri na unasihi katika shule za sekondari kwa kuwa na walimu na malezi na kuanzishwa kwa klabu za wasichana katika shule zote za Sekondari kwa mantiki ya kupunguza utoro na mimba za utotoni.

Wilaya hiyo ina jumla ya shule za sekondari 37 kati ya hizo za Serikali ni 35 na binafsi mbili na shule za msingi 159 zenye wanafunzi 68,316.
Mwisho.
    

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Lindi Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa