Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Jasi (Gypsum) ni moja ya madini yanayopatikana nchini, yamekuwa yakitumika zaidi kwa shughuli za ujenzi.
Moja ya maeneo ambayo madini haya yanapatikana ni katika Kijiji cha Makangaga, wilayani Kilwa Mkoa wa Lindi.
Uchimbaji wa madini hayo katika kijiji hicho ulianza rasmi mwaka 2006 na bado unaendelea.
Hadi sasa kuna kampuni 12 zinazochimba jasi katika
 kijiji hicho, zikiwamo Go On, Anglo African Gypsum, Tanzania Gypsum, 
Pita Ludovick, Kimambo , Agnes & Michael , Kwanza Kilwa , Mazongela ,
 Kawina , Ruben Investment na Mdhs Investment zote za Dar es Salaam.
Hata hivyo baadhi ya wananchi wamekuwa 
wakilalamikia uchimbaji huo kuwa umesababisha uharibifu mkubwa wa 
mazingira, hasa kwa vyanzo vya mto Makangaga hivyo kuharibu ukuaji na 
mazalia ya samaki.
Kwa kuzingatia uharibifu huo wa mazingira mwaka 
2012 aliyekuwa Naibu Waziri wa Nishati na Madini, George Simbachawene 
alifanya ziara katika Mkoa wa Lindi na kujionea hali hiyo ya uharibifu 
na kusimamisha uchimbaji hadi wachimbaji wafanye mazungumzo na kijiji.
Hata hivyo hadi sasa wachimbaji wanaendelea na kazi bila suluhu na wanakijiji.
Athari za mazingira na uchumi.
Baadhi ya wananchi wanaoishi katika kijiji hicho 
wametoa ushuhuda wao wakisema kabla ya uchimbaji huo kulikuwa na maji 
mengi, sasa mto huo umepungua kwa kiasi kikubwa hivyo kutishia 
upatikanaji wa maji siku za usoni.
Selemani Lingumbe, Mkazi wa kijiji hicho anasema kuwa hapo awali mto huo ulikuwa na maji mengi.
Lakini siku zinavyozidi kusonga mbele maji yake 
yamekuwa yakipungua kutokana na baadhi ya kampuni kuchimba madini hayo 
pembezoni mwa mto huo licha ya kwamba walishalalamikiwa na wanakijiji.
Shughuli za uchimbaji zinafanyika karibu na kuharibu mto huo, pia maji yake huchafuliwa kutokana na ufuaji wa nguo na kuoga.
“Wananchi hao wamekuwa wakifanya vitendo hivyo licha ya kujua 
kuwa maji hayo yanatumiwa na wakazi wa kijiji hicho chenye jumla ya watu
 4245,” anasema Lingumbe na kuongeza:
“Mto huu ni wa muda mrefu na umekuwa chanzo cha 
maisha yetu na uchumi wetu kwani pamoja na mambo mengine maji ya mto huu
 tunayatumia kwa kilimo cha umwagiliaji wakati wa kiangazi. Hivyo 
kupungua kwa maji haya kunaaathiri pia shughuli za kiuchumi. Serikali 
inapaswa kuwachukulia hatua kali baadhi ya kampuni zinazochimba madini 
karibu na vyanzo vya mito.”
Naye Mohamed Mnonya (53) anasema: “Sisi wanakijiji
 cha Makangaga tunashida sana maana hawa wachimbaji hawasikii. Wamekuwa 
wakiendelea kuchimba madini karibu na mto ambao unazidi kukauka. 
Serikali inajua hilo lakini haifuatilii kabisa,” anasema na kuongeza:
“Tangu mwaka 2006 wachimbaji hao walipoanza 
uchimbaji wa madini, tumeshuhudia kupungua kwa maji ya mto na bila hatua
 yoyote kuchukuliwa na Serikali.”
Kwa upande wake Hamisi Mbegwa ambaye shughuli zake
 ni kilimo anasema wakati wa kiangazi huwa analima kilimo cha 
umwagiliaji kwa kutumia maji ya mto huo. Lakini mazao yake sasa 
yamepungua kutokana na kushindwa kupata maji ya kutosha kwa ajili ya 
kilimo chake cha umwagiliaji.
“Nilikuwa nalima ekari tatu za mpunga kipindi cha 
nyuma na kupata gunia karibu 60 kama nimelima kitaalamu. Lakini kuanzia 
mwaka 2012, nimelima ekari moja tu na mwaka huu siwezi kulima kwa sababu
 ya upungufu mkubwa wa maji,” anasema.
Naye Selemani Matajiri, mkazi wa eneo hilo 
anabainisha kuwa hali ya afya za wananchi wa kijiji hicho zipo hatarini 
kutokana na wachimbaji hao kujenga vibanda vyao vya kulala karibu na 
mto;
“hatuvioni vyoo walivyojenga, kitu kinachofanya 
kuamini wanajisaidia pembeni ya huo mto na kufanya shughuli zingine 
ikiwamo kufua nguo. Unadhani tutapona na magonjwa? Hapa tutaugua tu hata
 kama siyo leo(sasa), basi miaka inayokuja maana magonjwa mengine 
yanachukua muda kujitokeza,” anasema Matajiri.
Kwa upande wake, Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha 
Makangaga, Muhidin Mkunguru amekiri kuwapo kwa tatizo hilo na kusema mto
 umepungua kwa kiasi kikubwa.
“Tangu nihamie kijijini hapa mwaka 2011, maji 
yalikuwa yanafika kiunoni. Lakini sasa maji yanafika chini ya magoti. 
Maji ya mto huo yanazidi kupungua na ndiyo tegemeo kubwa katika kijiji 
chetu chenye jumla ya vitongoji vinne vya Makangaga mjini, Mpindiro, 
Mageuzi na Kikundi,” anasema Mkunguru.
Kuhusu suala la kilimo, Mkunguru anasema katika 
kijiji hicho chenye wakazi wapatao 4245, wanalima mpunga, ufuta na 
mahindi. Na wakati wa kiangazi, wanajihusisha na kilimo cha umwagiliaji 
kwa kutumia huo mto na hupanda tena mpunga na kulima bustani za nyanya.
                
              Naye Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji cha 
Makangaga, Zainabu Mcheni anasema ni kweli watu hao wameharibu sana mto 
na kwamba licha ya Serikali kupata taarifa juu ya uharibifu huo, bado 
imekaa kimya hata baada ya kuwaamuru wachimbaji hao kuacha kuchimba 
karibu na mto Septemba 26, mwaka jana
“Kwa kweli maji yamepungua na kampuni hizi hazina ushirikiano 
kabisa na sisi. Wanachukua mali hapa kwetu kijijini lakini sisi wenyewe 
hawatupendi maana wanajua wanaharibu mto ambao ndiyo tegemeo letu,” 
anasema na kuongeza:
“Tunalia na Serikali kwa nini imekaa kimya kiasi 
hiki. Viongozi wa vijiji tunapata shida kutokana na kuulizwa mara kwa na
 wananchi juu ya hatma ya tatizo hili. Wananchi wanatuona kama hatufanyi
 kazi. Sisi tutafanya nini huku chini wakati Serikali iko kimya,” 
anasema Zainabu.
Kaimu Mganga wa Afya wa Zahanati ya kijiji cha 
Makangaga, Hamisi Kachwichwi anasema ni kweli mto umeharibiwa lakini 
hadi sasa bado zahanati yake haijapokea wagonjwa walioathirika kutokana 
na matumizi ya maji yaliyoharibiwa na shughuli za uchimbaji wa madini.
Naye Kaimu Ofisa Mazingira wa Wilaya ya Kilwa, 
Raymond Cholobi hakuwa tayari kuzungumzia utoaji wa cheti cha mazingira 
akidai kuwa hana mamlaka.
Kamishna wa Madini Kanda ya Kusini, Mhandisi Benjamin Mchwampaka anasema kuwa bado hajapata taarifa za kuhusu mradi huo.
“Suala hili bado halijaletwa hapa ofisini kwangu. 
Halijafika bado, sijaliona wala kulisikia hivyo nawashauri wakazi wa 
kijiji hicho kuleta taarifa hiyo ofisini kwangu ili hatua za haraka 
zichukuliwe,” anasema Mchawampaka.
Kwa upande wa Ofisa Misitu na Mazingira mkoani 
Lindi, Zawadi Jilala amekiri kuwapo kwa uharibifu wa mazingira katika 
eneo hilo na kwamba sheria ya mazingira imekiukwa:
“Sheria ya mazingira ya 2004 (Environmental 
Management Act, 2004) inatamka wazi kuwa shughuli zozote za kibinadamu 
zifanyike nje ya mita 60 toka kwenye chanzo cha maji. Ukiwa kama mto, 
visima, bwawa, hao wamekiuka hiyo sheria, nashangaa uongozi wa Serikali 
ya kijiji upo kimya kiasi hicho, wakati wanajua hilo ni tatizo kubwa 
litakalo waathiri hapo baadaye,” alisema Jilala.
Mratibu wa Mtandao wa Jamii wa Usimamizi wa Misitu
 Tanzania- Mjumita- Akrei Arbat anasema licha ya kutokufika katika eneo 
hilo, ameshasikia malalamiko ya wananchi na viongozi wa halmashauri 
wakilizungumzia.
“Wamekiuka sheria ya mazingira ya 2004 kwa makusudi.”
Anasema ingekuwa jamii tungesema haina uelewa, 
sasa hao wasomi kabisa watakuwa ni wajeuri tu, lakini Serikali iwaondoe 
maana huo mto ukikauka itakua shida kwa wakazi wa kijiji hicho,” anasema
 Akrei.
Mkuu wa Wilaya ya Kilwa, Abdallah Ulega amekiri 
kuwapo kwa tatizo hilo katika Kijiji cha Makangaga la kuharibu mto 
unaofanywa na wachimbaji wa madini ya jasi.
 “Nimewahi kuzungumza nao, nitakwenda kuzungumza nao tena ili waweze 
kuondoka na kama watakaidi itabidi tutumie nguvu,” anasema na kuongeza 
“Cha msingi mimi nashauri hizo mamlaka za juu ziingilie kati suala hilo 
kwa nguvu”.
chanzo;Mwananchi 
 
 
 
 
 
0 comments:
Post a Comment