Home » » MAUAJI KINYAMA YA WANAWAKE YATIKISA

MAUAJI KINYAMA YA WANAWAKE YATIKISA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Lindi, Renatha Mzinga
 
Kundi la wananchi wamevamia kituo cha polisi cha Nachingwea mkoani Lindi na kwa Mkuu wa Wilaya hiyo, Regina Chonjo kulalamikia askari wa jeshi hilo na serikali kushindwa kuwasaidia ndugu zao wa kike dhidi ya vitendo vya kinyama, ikiwamo kubakwa, kuuawa na  kunyofolewa sehemu za siri.
Kamanda wa  Polisi Mkoa wa Lindi, Renatha Mzinga, amethibitisha kuwapo na matukio hayo na kukanushwa maiti zote kukutwa zimenyofolewa sehemu za siri.

Hatua ya wakazi hao ilikuja baada ya mwanamke aliyekuwa mkazi wa Mtaa wa Mianzini kukuta ameuawa na watu bado hawajafahamika na mwili wake kutupwa katika eneo la nyumba mpya ya wageni inayopo jirani na inayoendelea nyinghine inayoendelea kujengwa.

Inadaiwa kuwa mwanamke huyo ni wa nne kuuawa wilayani humo tangu Mei, mwaka huu.
Habari hizo zinaeleza kuwa kabla ya kumuua, wauaji walimlaza chali, huku wakiwa wamemvua nguo zote na kubaki utupu na kisha kumbaka.

Hali hiyo iliibua hasira kutoka kwa wananchi hao, ambao waliamua kufanya maandamano na kuzingira kituo hicho cha polisi na nyumbani kwa mkuu huyo wa wilaya.

Mmoja wa wananchi hao alidai kuwa  walifikia hatua hiyo ili kuwasilisha malalamiko yao kutokana na kukithiri kwa vitendo hivyo vya kinyama bila vyombo vya usalama wala serikali kuwakamata watuhumiwa.

Aliitaja sababu nyingine kuwa ni kutokana na mwili wa marehemu  huyo kuchelewa kuondolewa katika eneo ulikotupwa.

Wakati baadhi ya wananchi hao wakimbia nyumbani kwa  kwa Mkuu wa Wilaya hiyo, Regina Chonjo, lakini hawakufanikiwa kumkuta.

Inaelezwa kuwa Chonjo alikuwa safarini mjini Lindi kuhudhuria kikao cha maandalizi ya maonesho ya ya kilimo maarufu kama Nanenane, ambayo kitaifa mwaka huu yanafanyika mkoani Lindi.

Chonjo alipoulizwa na NIPASHE, alithibitisha kuwapo kwa vurugu hizo, lakini hakuwa tayari kuzungumza kwa kirefu.
“Ni kweli vurugu hizo zimetokea, lakini nashindwa kuzielezea zaidi, kwani na mimi nimepata taarifa hii nilishaondoka kuja hapa Lindi kuhudhuria kikao cha Nanenane,” alisema Chonjo.

Alisema kutokana na tukio hilo, amelazimika kukatisha kuendelea na kikao hicho na kurejea Nachingwea.

Wakizungumza na NIPASHE kwa nyakati tofauti jana, wakazi hao walidai kuwa ndugu zao, ambao ni wasichana wenye umri chini ya miaka 30, wamekuwa wakifanyiwa unyama huo na kwamba, hadi kufikia jana, wanane walikuwa wamekwishauawa.

“Tumechoshwa sisi. Kila kukicha unakuta msichana mmoja kafa, huku wamemkata maumbile yake ya sehemu za siri na...,” alidai kwa uchungu mmoja wao.

Aliongeza: “Tumeishalalamika kwa Jeshi la Polisi. Mpaka sasa wanaofanya vitendo hivyo bado hawajakamatwa.”
Walidai mwaka jana waliuawa wasichana wawili na kwamba,  ndani ya mwezi huu watano.

Wakazi hao walidai alfajiri jana, aliuawa mwanamke huyo ambaye ameacha mtoto mchanga na watu hao wasiojulikana.
Walidai kinachowaumiza ni mauaji hayo kufanyika, lakini polisi hawawapi ushirikiano na ndiyo maana wamelazimika kuvamia kituo hicho na nyumbani kwa mkuu wao wa wilaya.

Katibu wa Chama cha ADC Wilaya ya Lindi, Moshi Mataka alisema wamechoshwa na matukio hayo.Alisema wamelalamika, lakini mpaka sasa hakuna kinachoendelea juu ya kuwachukulia hatua watuhumiwa.

 Mataka alisema wameanza kufanya vikao kuelimishana na wananchi juu ya kupambana na watu hao, ambao wanawafanyia wasichana vitendo vibaya.
“Tunataka kuandaa ulinzi shirikishi ili kudhibiti hali hii, ambayo imekuwa inajitokeza kila mara,” alisema Mataka.

Mchukua Kumbukumbu za Wilaya hiyo, Shakili Bhimi alisema wanawake 10 wameuawa kwa kubakwa na kunyofolewa sehemu zao za siri.

Alisema pamoja na kunyofoa sehemu za siri, pia wanawanyofoa vitu vya uzazi kwa ajili ya kuvipelekwa kwa waganga wa jadi kupata madini ya dhahabu kwa wingi.
“Mwaka jana waliuawa wasichana wawili na mwaka huu wameuawa wasichana nane na idadi hiyo inakuwa ni jumla ya wasichana 10,” alisema Bhimi.
Akizumgumzia kuhusu wananchi kukosa ushirikiano wa polisi, Kamanda Mzinga alikanusha akisema wao  ndiyo wanaokosa ushirikiano wao.

“Unajua hivyo ni visasi vinatoka kwa hao hao wananchi. Kama mtu kaolewa na kuachana na mumewe na kuolewa kwingine, ndio hivyo. Mtu aliyeachwa anamvizia msichana na kufanya mauaji hayo. Hili sisi tulilijua baada ya kuwakamata mwaka jana watu wawili na kuwahoji,” alisema Kamishna Msaidizi Mzinga.

Alisema mwaka jana waliuawa wasichana wawili na walipowahoji wananchi ndipo walipopata ushirikiano wa kuwakamata watuhumiwa, ambao alisema mpaka sasa wapo makahamani wana kesi za kujibu.

Pia alikanusha maiti wote wanaokutwa wanakuwa wamekatwa sehemu za siri.Alisema maiti wengi wamekuwa wakibakwa na ni mmoja tu wa juzi ndiye alikutwa akiwa amekatwa sehemu za siri huku ikiwa zikiwa zimetiwa miti.

Pia alisema walilazimika kutumia mabomu ya machozi kuwatawanya wananchi waliovamia kituo hicho na kwamba, hakuna mali yoyote katika ofisi hiyo iliyoharibika wala raia aliyepata majeraha katika tukio hilo.

Alisema mpaka sasa ni watu saba waliouawa katika vitendo hivyo vya kinyama, wakiwamo wawili  mwaka jana, watano mwaka huu.

Hata hivyo, alisema polisi wameanza kuingia katika maeneo mbalimbali ya vijiji kuwasaka na kuwakamata waliohusika na mauaji hayo.
SOURCE: NIPASHE

0 comments:

 
Supported by Tone multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Lindi Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa