Home » » ‘Miji irembwe kuinua utalii’

‘Miji irembwe kuinua utalii’

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Tumekuwa tukiandika kwa muda mrefu sana kuhimiza utalii wa ndani na wageni kutoka nje. Pia kuhusu umuhimu wa kuzilinda rasilimali na amali zetu za kiutamaduni na kihistoria na kimazingira (wanyama na misitu). Kwa ufupi nitaeleza utalii unaweza kuwa na faida gani kwa jamii na taifa.
Utunzaji wa mazingira na uoto kwa ajili ya utalii licha ya kuliingizia Taifa fedha za ndani na za kigeni kwa kutokana na wageni watembeleao vivutio. Lakini utunzaji huo husaidia pia kuleta mvua na kutunza maji ambavyo ni muhimu kwa wakulima na wafugaji. Kwa hiyo utalii huweza kuwa na faida kwa njia ya namna hiyo ya mzunguko kwa wananchi na kukuza hali ya kipato chao katika shughuli zisizo za kitalii.
Ni muhimu sana kwa Serikali kujenga miundombinu inayosaidia kukuza utalii, lakini wananchi wanaweza kuwa na jukumu kubwa zaidi la kuimarisha miundombinu kama usafiri, nyumba za kulala wageni au sehemu za burudani (kambi za utalii, mikahawa na vyakula vya kiasili) kwa ajili ya kuwavutia watalii. Tanzania imebarikiwa sana na vivutio vya utalii ambavyo havitumiwi, kama wananchi wangejishirikisha vizuri ingekuwa rahisi kwa nchi kuvitunza na kuviuza vivutio vya utalii. Mto Pangani, kwa mfano, unaweza kutumika vizuri sana kwa ajili ya Utalii wa kihistoria na wa kimazingira. Wananchi wanaweza kuhamasishwa kuwekeza katika miundombinu hasa usafiri na maeneo ya kujihifadhi na kuwasafirisha watalii kwenye mto kuona mazingira na maeneo ya kihistoria. Maeneo ambayo wananchi wameshirikishwa vizuri faida ya utalii kwa jamii huonekana wazi, ili mradi ushirikishwaji huo usiwe wa kudhalilisha mila na desturi zetu. Lakini hapa tunaona utalii ukiongeza ajira binafsi kwa wakazi. Unguja mjini inatoa mfano mzuri kwa hivi karibuni vijana kuanzisha miradi ya usafirishaji wa watalii kwenda kwenye visiwa vyenye vivutio vya utalii vilivyo jirani.
Watalii huja eneo fulani kutafuta vitu ambavyo kwao hawana, au kula vyakula ambayo kwao havipo, na kuburudika kwa ujumla. Kwa kuweza kupata hayo wanayotafuta kutoka maeneo ya utalii, nchi wapokeaji watalii hulazimika kukuza ubora wa vyakula, au ubora wa maeneo ya kulala ili kuweza kufikia viwango vya kimataifa.
Kwa njia hiyo utalii hukuza uchumi na kukuza tabia za usafi, kuhimiza ujenzi wa kisasa wa majengo, au kuwa na huduma za kisasa katika maeno fulani fulani ili kuwavutia watalii na hivyo kuongeza ajira. Tumesema kuwa kama nchi inajipanga vizuri katika utalii kuna uwezekano wa kukuza aina fulani ya vyakula, hasa matunda na mbogamboga ambavyo watalii huvipenda sana.
Matunda kama tufa, machungwa na ndizi, na mengine yasiyo na asili ya Ulaya hupata soko sana maeneo ya utalii. Kwa hili serikali hulazimika kuweka sera nzuri za kilimo na kuhamasisha ulimaji mazao ambayo yanayoweza kuongeza pato la wananchi kupitia watalii.
Kwa sasa hivi mifumo ya utangazaji ndani na nje ya nchi haina uchagamano unaoweza kuleta tija.
Ni bora kama watalii wanapokuwa wanatembelea nchi wakajua kuwa pamoja na kuona utalii wa wanyama, kwa mfano, bado kuna maeneo ya historia yaliyo jirani. Pia wananchi wana utamaduni wao ambao wangeweza kuwaonyesha au kuwauzia wageni.
Kwa vile wananchi wengi walio katika maeneo ya utalii hawajahamasishwa hawaelewi namna gani wanavyoweza kujiingiza katika shughuli ambazo wangewauzia watalii.
Bagamoyo kwa mfano, wangeweza kuhamishwa kujiunga katika shughuli za upikaji chakula, au uchezaji na kurekodi ngoma za asili kwa ajili ya watalii. Wananchi wamebaki nao wakiwa waangaliaji watalii wanaotembelea maeneo yao bila kupata faida ya moja kwa moja kupitia shughuli ambazo wangezifanya.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Lindi Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa