Home » » Wanakijiji Mirumba wafunga barabara

Wanakijiji Mirumba wafunga barabara

WANAKIJIJI cha Mirumba, Wilaya ya Kilwa, Lindi walilazimika kufunga barabara kwa kupanga mawe na magogo baada ya watoto wawili kugongwa na gari wakati wakivuka barabara na kusababisha kifo cha mmoja wao.
Watoto waliogongwa na gari aina ya Fuso ambalo namba zake hazikupatikana ni Celina Anthony, aliyefariki dunia papo hapo na Theresia Bernard, alijeruhiwa sehemu mbalimbali za mwili wake.
Kitendo cha wanakijiji hao kufunga barabara kilisababisha usumbufu ambapo abiria zaidi ya 1,000 walikwama kuendelea na safari zao kwa zaidi ya saa nne.
Baadhi ya wakazi wa kijiji hicho Musa Juma, Halima Hassan, Mwajuma Saidi na Bakari walisema wameamua kufunga barabara ili kuishinikiza serikali kupitia Wakala wa Barabara nchini (Tanroads) kuweka matuta kupunguza ajali kijijini hapo.
“Ukweli tunateseka na barabara hii, tunahatarisha maisha yetu wakati wa kuvuka barabara kwani magari yamekuwa yakikimbia mno wala hawajui kama kuna kijiji wapunguze mwendo kwenye makazi ya watu, watoto wetu wanagongwa na kufa wengine wanabaki walemavu lakini serikali ipo kimya na tatizo hili ni la muda mrefu wanalijua,” walisema wanakijiji hao.
Suluhu ya vurugu hizo ilipatikana baada ya ombi la Mkuu wa Polisi wa Wilaya ya Kilwa, Yahya Mdogo, kuwataka wananchi hao kuwa na subira huku akiwashauri kuondoa magogo na mawe ili magari yapite.
Rashid Mohamed na Ephrem Ndunguru, madereva wa mabasi yaendayo mikoa ya Kusini mwa Tanzania walilalamikia kitendo cha askari wa Usalama Barabarani kukaa msituni badala ya maeneo ya vijiji yenye msongamano wa watu.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Lindi, George Mwakajinga, amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo na kuwataja watoto waliogongwa kuwa ni Celina Anthony (7) aliyefariki dunia papo hapo na Theresia Bernard alijeruhiwa.
Kamanda Mwakajinga alisema ajali hiyo ilitokea Oktoba 4, mwaka huu saa tano asubuhi na kwamba dereva wa gari lililosababisha ajali, Seif Ruanda, alijisalimisha Kituo cha Polisi Lindi kwa usalama wake.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Lindi Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa