Home » » TUMEANZA KUIONJA SHUBIRI YA VITA YA UCHUMI.

TUMEANZA KUIONJA SHUBIRI YA VITA YA UCHUMI.


Na Bashir Yakub. 

Tumegusa uchumi wa bepari. Mara zote, na kote duniani bepari alipoguswa kwenye uchumi wake basi ametumia mbinu hizi hapa chini kuhakikisha anapambana na waliomzuia.

[a] Kumwita kiongozi anayeongoza vita ya uchumi Mvunjaji wa haki za binadamu na asiyefaa. Imetokea kwa Gaddafi baada ya kumnyima bepari mafuta, halikadhalika kwa Saddam Hussein.Pia ndilo tatizo la Mugabe na bepari baada ya kurudisha mashamba kwa wazawa ili wafaidi uchumi wao.

[b] Kuratibu na kufanikisha matukio ya ajabu kwenye jamii ili kuleta faraka,taharuki, chuki, uadui, na sintofahamu.Bepari analiweza sana hili hasa nchi za Afrika kutokana na uwezo wake mkubwa wa fedha na teknolojia.

Lengo la mbinu hii ni :
Mosi,kuwatoa kwenye ajenda ya vita dhidi yake na kuwaelekeza kwenye mijadala mingine.
Pili, kuchonganisha watu, serikali na viongozi wao.
Tatu, kupeleka ujumbe duniani kuwa kiongozi fulani na serikali yake hawafai tena.
Nne, kuligawa taifa kati ya upande unaoamini matukio kutekelezwa na fulani na upande unaoamini vingine.

[c] Kuandaa mapinduzi kwa kuwatumia wasaidizi wa rais na viongozi wenye tamaa.

[d] Kuandaa maandamamo makubwa ambayo mwisho wake ni kuuondoa utawala uliodhibiti uchumi .

Utaona waandamanaji wanalalamika kuchoshwa na mambo mbalimbali lakini nyuma yao ni fedha, mbinu na mipango ya bepari.

Bila hata waandamanaji kujua isipokuwa wachache/viongozi wao. Mbinu hii imetumika hivi karibuni kuondoa viongozi wengi wa Afrika ya Kaskazini waliodhibiti uchumi wao kwa mda mrefu.

[e] Kufadhili makundi ya waasi Mf. Congo, Sudani Kusini, Sierra Leone, Liberia nk. Mnajua kuwa hadi baadhi ya makundi ya kigaidi hufadhiliwa na hawa jamaa.

Badala ya kujadili udhibiti wa rasilimali zenu mnajadili amani itapatikana vipi huku bepari akitumia nafasi hiyo kuiba.

[f] Kufadhili na kuviimarisha vyama vya upinzani hasa vyenye tamaa ili hatimaye na kwa namna yoyote ile viondoe madarakani viongozi waliombana bepari.

[g] Kutafuta sababu na hatimaye kuweka vikwazo vya kiuchumi kwa nchi husika ili kulainisha au kumaliza kabisa misimamo ya serikali na viongozi dhidi ya rasirimali anazozitaka bepari.

Pia lengo ni kuwafanya wananchi wapate taabu ili wachoshwe na utawala uliombana bepari na hivyo kufanya maamuzi ya kuuondoa kwa namna yoyote. nk, nk, nk............


NINI MFANYE KTK KIPINDI KAMA HIKI.


[a] Kushikamana na kutokubali kutenganishwa kwa matukio.

[b]Kutokuwa na majibu ya haraka katika mambo makubwa.

[c] Vyombo vya usalama kujiimarisha kiulinzi na kuhakikisha vinafika kwenye majibu ya mzizi wa kila tukio na kutoa taarifa kwa wakati kwa umma.

[d] Vyombo vya usalama kutokubali kusaidiwa upelelezi na nchi za mabepari kwakuwa mwanya huo hutumika kutoa majawabu aidha yanayokwepesha(divert) ukweli au yanayokamilisha malengo yaliyokusudiwa.

[e] Kuepuka kabisa kuchanganya tofauti zetu za kisiasa za tokea huko nyuma na yanayotokea sasa.

YAPI MADHARA YA KUTOSHIKAMANA KIPINDI KAMA HIKI.

Bepari hana hasara, wenye hasara ni mimi na wewe. Mpango wa wagawe uwatawale "divide&rule" haikuishia kwenye ukoloni. Bado ungalipo.

Kama tutakubali kugawanywa na majaribu ya bepari , sawa na tugawanywe tu , ila ahadi ni hii kuwa kila mmoja ataonja joto la jiwe.

Wewe uliyekubali kugawanywa utaonja na ambaye hakukubali ataonja. Mtaona Iraq na Libya aliyeshiriki na ambaye hakushiriki wote wanaonja.

Hakuna atakayekuzuia kukomaa na msimamo wako. Hakuna atakayekuzuia  kuamini mbowe ndiye aliyefanya tukio fulani ili kumzuia fulani kugombea uenyekiti. Hakuna atakayekuzuia kuamini kuwa Lowassa ndiye aliyefanya tukio fulani ili kumzuia fulani kugombea urais 2020. Lakini pia hakuna atakayekuzuia kuamini kuwa serikali ndiyo iliyofanya tukio fulani kwasababu yule au ofisi ile kuna wabaya au wakosoaji wake. 

Wewe amini hivyohivyo unavyoamini ila kaa ukijua kuwa ikiwa tutagawanyika tu, basi kila mtu, kila familia, kila kundi, kila chama, na imani yako hiyohiyo uliyonayo yatakufika. Madhara ya bepari yanapokuja hayaangalii nani alikuwa akiamini nini, ama nani alitumia gani tukio kumsema nani. 

Mtaona Libya kusini ina serikali yake, kaskazini ina serikali yake , magharibi yake na mashariki yake.Ni vipandevipande, shida juu ya shida. Na humo wamo wote walioshiriki na ambao hawakushiriki. Madhara ya bepari hayaangalii aliyeshiriki na ambaye hakushiriki. 

Kwahiyo wewe msaidie tu bepari kwakujua au kutokujua kueneza propaganda zake kwa matukio anayoyaandaa ila ujue kuwa mwisho wa tamthilia tutakuwa wote tuu. Wala huna pa kwenda ndugu tutalia wote humuhumu. 

Na mkishakuwa nyang’anyang’a, bepari ameshawashinda, na hamna tena la  kumfanya, na sasa anawageuza anavyotaka, basi hapo bepari atakuja na kusema ukweli kuwa si fulani aliyefanya tukio fulani bali ni sisi kwa lengo fulani. 

Mnakumbuka wale walioiharibu Iraq baadae walisema ukweli. Waliandika vitabu kuwa vita ile ilikuwa ya makosa na kule hakukuwa na silaha za sumu kabisa. Ni baada ya kuiharibu vibaya sana nchi hiyo na kuiletea dhiki na mashaka makubwa.

Mnakumbuka walioiharibu Libya nao baadae walisema ukweli. Sasa wanasema wazi kuwa makundi waliyoyatumia kumg’oa Gaddaffi hayakuwa makundi sahihi bali ya imani kali. 

Lakini mwanzoni walikataa kuwa hawako nyuma ya makundi yaliyoanzisha  maandamano na kusema kuwa wananchi waliochoka udikteta wa Gaddaffi ndio wanaoandamana. Bepari akishakumaliza anakiri. Basi kwa kiwango gani mnakuwa mmedhalilika na kudharauliwa ndugu zangu. Ni lini wananchi wa Afrika tutajifunza kutoka matukio haya. 

Tunawalaumu viongozi wetu waafrika lakini pia sisi wananchi wa Afrika kwa nafasi zetu kama wananchi tunayo mambo ya kujifunza na kushughulikia lakini hatufanyi hivyo. Ni lini basi tutaacha kudhalilishwa na bepari. Toka ukoloni mpaka uhuru hatujifunzi tuu ndugu zangu. Basi tutajifunza lini , makaburini ama.

Tujihadhari kwani kwetu tayari bepari ameanza kwa matukio ya hapa na pale. Tukimuunga mkono kwa vinywa vyetu huku tukijua tunamkomoa kiongozi fulani au chama fulani, basi atatuvuta taratibu taratibu mpaka huko Libya na Iraq halafu yeye aendelee kuiba kama alivyokuwa amezoea awali.

Ndugu zangu, tunawasifia Angola na Botswana kwa kumbana bepari na hatimaye kufaidi rasimali zao sasa.

Lazima tujue wamefikia hapo baada ya kushikamana na kuzishinda hila, fisadi, fitna,na mitihani ya bepari. Na sisi tunaweza.


TUTARAJIE MATUKIO ZAIDI.

Matukio bado , huu ni mwanzo tu. Hivi mlitarajia bepari abanwe halafu tubaki salama. Haiwezekani. Historia inakataa jambo hilo. Bepari lazima akutingishe.

Kama ingekuwa tumbane bepari halafu tubaki
salama basi isingeitwa Vita ya Uchumi bali Sherehe ama tafrija ya Uchumi. Yanini iitwe vita kama mmembana bepari na bado mkaendelea kuwa salama na kufurahia maisha. Hii ni vita na sasa mnaweza kuanza kuona taswira ya vita yenyewe.

Vitimbi na matukio yatakuja mengi. Lengo ni moja tu , kuua vita hii ili bepari aendeleze alikoishia.

Msishangae wakaanza kudhuliwa hata wanaoonekana wana mtazamo tofauti na mwenyekiti ndani ya chama tawala ili chama kigawanyike na hatimaye serikali igawanyike. Bepari anajua ukigawa chama kinachotawala  umeigawa serikali kwakuwa wanachama wa chama tawala ndio huunda serikali.

Hivyo kwa kufanikiwa kukigawa chama kinachotawala bepari anajua atakuwa amefanikiwa kuigawa serikali.

Ukifanikiwa kuigawa serikali maana yake bepari amepunguza kasi ya vita dhidi yake lakini maana yake pia anakaribia kumwondoa kabisa adui aliyebana uchumi wake.

Bepari haoni tabu kumdhuru yeyote ama chochote ili kutimiza malengo yake. Bepari anajua ukimdhuru kiongozi mwenye mawazo tofauti ndani ya chama ama serikali , basi watanyoosheana vidole. Yule aliyedhuriwa atapata kundi lake wanaoamini ameonewa na wale wengine watabaki kundi jingine. Bepari  anajua kuwa hata kiongozi awe mkali ama na msimamo kiasi gani hawezi kusimama kama wasaidizi wake wamegawanyika. 

Ni vita ya uchumi , na sasa tunaonja shubiri yake. Ila tutashinda.


MWANDISHI WA MAKALA HAYA NI MWANASHERIA NA MCHAMBUZI WA MASUALA YA SIASA. 0784482959.
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Lindi Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa