Benny Mwaipaja, WFM, 
Kampuni
 moja ya Ujerumani ya Ferrostaal, inatarajia kujenga kiwanda kikubwa cha
 mbolea katika wilaya ya Kilwa mkoani Lindi, kitakacho gharimu zaidi ya 
Euro Bilioni 1 nukta 2 (1.2bln) ambacho kinatajwa kuwa kitakuwa moja ya 
viwanda vikubwa vya mbolea Barani Afrika.
Hayo
 yamesemwa na Balozi wa Ujerumani hapa nchini, EGON KOCHANKE, wakati 
alipomtembelea na kufanya mazungumzo na Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt.
 Philip Mpango, Jijini Dar es salaam, ambapo wawili hao wamezungumzia 
masuala kadha wa kadha yanayohusu uhusiano kati ya Tanzania na Ujerumani
 uliodumu kwa muda mrefu.
Balozi
 Kochanke amesema kuwa kiwanda hicho kitakachojengwa kwa ubia kati ya 
kampuni hiyo ya Ujerumani na wawekezaji wazawa na wengine kutoka Bara la
 Asia, inatokana na  hamasa kubwa ya serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Dkt. John Pombe Magufuli katika kuhamasisha ujenzi wa viwanda.
“Kiwanda
 hiki kitakuwa kikubwa zaidi ya mara mbili ya kiwanda cha saruji cha 
Dangote kilichoko Mtwara na kitagharimu Euro Bilioni 1.2, kitasisimua 
uchumi wa nchi pamoja na kukuza ajira” alisema balozi huyo aliyeambatana
 na naibu Balozi wa Ujerumani hapa nchini, John Reyels na Mkurugenzi wa 
Ushirikiano wa nchi hiyo Julia Hannig. 
“Mbali
 ya Kampuni hiyo ya Ferrostaal, wawekezaji wengine ni kampuni ya Mbolea 
ya Minjingu, na kampuni nyingine kutoka Pakistan ambayo kwa pamoja 
wameingia ubia wa kujenga kiwanda hicho cha mbolea kitakachokuwa 
uwekezaji mkubwa” Aliongeza Balozi Egon Kochanke.
Egon
 Kochanke, ameiomba serikali kutatua changamoto ya gharama za gesi ili 
kiwanda hicho kiweze kuanza ujenzi wake mapema iwezekanavyo na kuchochea
 maendeleo ya kilimo hapa nchini.
Ameyataja
 maeneo mengine ambayo nchi yake itaelekeza rasilimali zake kuwa ni 
kuendeleza sekta ya afya, wajasiriamali wadogowadogo, sekta ya ufundi 
mchundo pamoja na kuhamasisha wawekezaji kutoka nchini mwake kuja 
kuwekeza viwanda na biashara mbalimbali hapa nchini.
Aidha,
 Balozi huyo wa Ujerumani ameahidi kuwa nchi yake iko tayari kutoa kiasi
 kikubwa cha fedha ili kuifanyia ukarabati meli ya MV Liemba, inayofanya
 zafari zake katika ziwa Tanganyika, ambayo ni meli ya kihistoria kwa 
kuwa na umri wa zaidi ya miaka 100, ili iweze kuendelea kutoa huduma kwa
 watanzania na nchi jirani za Zambia, Burundi na DRC Kongo.
Kwa
 upande wake Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango, ameishukuru
 Ujerumani kwa ushirikiano mzuri uliopo kati ya nchi hizo mbili na 
kwamba Tanzania iko tayari kuendeleza ushirikiano huo. 
Amesema
 kuwa uwekezaji wa kiwanda kikubwa na cha mfano cha mbolea huko mkoani 
Lindi, utachochea sekta ya kilimo ambayo inaajiri zaidi ya asilimia 75 
ya watanzania, kwa kuongeza tija ya uzalishaji wa mazao ya wakulima na 
mbolea ya ziada itauzwa nchi za nje.
Dkt.
 Mpango, amemshukuru Balozi huyo wa Ujerumani kwa ahadi yake ya kusaidia
 kukarabati meli ya MV Liemba, na kiomba nchi hiyo kusaidia ununuzi wa 
meli mpya ili kuimarisha usafiri na usafirisha wa watu na mizigo katika 
eneo la maziwa makuu.
Vilevile
 ameiomba nchi hiyo kuendeleza misaada yake katika sekta ya ufundi 
kupitia mamlaka ya Ufundi Stadi (Veta) pamoja na kuendelea kutoa 
ufadhili wa masomo ya juu kwa wanafunzi wa kitanzania kwenda kusoma 
nchini humo kama ambavyo imekuwa ikifanya miaka mingi iliyopita kupitia 
Chuo Kikuu cha Dar es salaam.
Balozi
 Kochanke amekubali kufanya hivyo na kuahidi kuwa nchi yake iko tayari 
kushirikiana na Tanzania katika mambo hayo na masuala mengine, ikiwemo 
kuishauri namna bora ya kuhamishia Serikali mkoani Dodoma, wakitumia 
uzoefu wa nchi hiyo ilipohamisha makao makuu yake kutoka Berlin kwenda 
Born.
 

 
 
 
 
0 comments:
Post a Comment