Home » » KIWANDA KIKUBWA CHA MBOLEA KUJENGWA MKOANI LINDI

KIWANDA KIKUBWA CHA MBOLEA KUJENGWA MKOANI LINDI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Benny Mwaipaja, WFM,
Kampuni moja ya Ujerumani ya Ferrostaal, inatarajia kujenga kiwanda kikubwa cha mbolea katika wilaya ya Kilwa mkoani Lindi, kitakacho gharimu zaidi ya Euro Bilioni 1 nukta 2 (1.2bln) ambacho kinatajwa kuwa kitakuwa moja ya viwanda vikubwa vya mbolea Barani Afrika.
Hayo yamesemwa na Balozi wa Ujerumani hapa nchini, EGON KOCHANKE, wakati alipomtembelea na kufanya mazungumzo na Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango, Jijini Dar es salaam, ambapo wawili hao wamezungumzia masuala kadha wa kadha yanayohusu uhusiano kati ya Tanzania na Ujerumani uliodumu kwa muda mrefu.
Balozi Kochanke amesema kuwa kiwanda hicho kitakachojengwa kwa ubia kati ya kampuni hiyo ya Ujerumani na wawekezaji wazawa na wengine kutoka Bara la Asia, inatokana na  hamasa kubwa ya serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Dkt. John Pombe Magufuli katika kuhamasisha ujenzi wa viwanda.
“Kiwanda hiki kitakuwa kikubwa zaidi ya mara mbili ya kiwanda cha saruji cha Dangote kilichoko Mtwara na kitagharimu Euro Bilioni 1.2, kitasisimua uchumi wa nchi pamoja na kukuza ajira” alisema balozi huyo aliyeambatana na naibu Balozi wa Ujerumani hapa nchini, John Reyels na Mkurugenzi wa Ushirikiano wa nchi hiyo Julia Hannig.
“Mbali ya Kampuni hiyo ya Ferrostaal, wawekezaji wengine ni kampuni ya Mbolea ya Minjingu, na kampuni nyingine kutoka Pakistan ambayo kwa pamoja wameingia ubia wa kujenga kiwanda hicho cha mbolea kitakachokuwa uwekezaji mkubwa” Aliongeza Balozi Egon Kochanke.
Egon Kochanke, ameiomba serikali kutatua changamoto ya gharama za gesi ili kiwanda hicho kiweze kuanza ujenzi wake mapema iwezekanavyo na kuchochea maendeleo ya kilimo hapa nchini.
Ameyataja maeneo mengine ambayo nchi yake itaelekeza rasilimali zake kuwa ni kuendeleza sekta ya afya, wajasiriamali wadogowadogo, sekta ya ufundi mchundo pamoja na kuhamasisha wawekezaji kutoka nchini mwake kuja kuwekeza viwanda na biashara mbalimbali hapa nchini.
Aidha, Balozi huyo wa Ujerumani ameahidi kuwa nchi yake iko tayari kutoa kiasi kikubwa cha fedha ili kuifanyia ukarabati meli ya MV Liemba, inayofanya zafari zake katika ziwa Tanganyika, ambayo ni meli ya kihistoria kwa kuwa na umri wa zaidi ya miaka 100, ili iweze kuendelea kutoa huduma kwa watanzania na nchi jirani za Zambia, Burundi na DRC Kongo.
Kwa upande wake Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango, ameishukuru Ujerumani kwa ushirikiano mzuri uliopo kati ya nchi hizo mbili na kwamba Tanzania iko tayari kuendeleza ushirikiano huo.
Amesema kuwa uwekezaji wa kiwanda kikubwa na cha mfano cha mbolea huko mkoani Lindi, utachochea sekta ya kilimo ambayo inaajiri zaidi ya asilimia 75 ya watanzania, kwa kuongeza tija ya uzalishaji wa mazao ya wakulima na mbolea ya ziada itauzwa nchi za nje.
Dkt. Mpango, amemshukuru Balozi huyo wa Ujerumani kwa ahadi yake ya kusaidia kukarabati meli ya MV Liemba, na kiomba nchi hiyo kusaidia ununuzi wa meli mpya ili kuimarisha usafiri na usafirisha wa watu na mizigo katika eneo la maziwa makuu.
Vilevile ameiomba nchi hiyo kuendeleza misaada yake katika sekta ya ufundi kupitia mamlaka ya Ufundi Stadi (Veta) pamoja na kuendelea kutoa ufadhili wa masomo ya juu kwa wanafunzi wa kitanzania kwenda kusoma nchini humo kama ambavyo imekuwa ikifanya miaka mingi iliyopita kupitia Chuo Kikuu cha Dar es salaam.
Balozi Kochanke amekubali kufanya hivyo na kuahidi kuwa nchi yake iko tayari kushirikiana na Tanzania katika mambo hayo na masuala mengine, ikiwemo kuishauri namna bora ya kuhamishia Serikali mkoani Dodoma, wakitumia uzoefu wa nchi hiyo ilipohamisha makao makuu yake kutoka Berlin kwenda Born.

0 comments:

 
Supported by Tone multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Lindi Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa