Home » » IPIGIENI KURA YA NDIYO KATIBA INAYOPENDEKEZWA - MAMA SALMA KIKWETE‏

IPIGIENI KURA YA NDIYO KATIBA INAYOPENDEKEZWA - MAMA SALMA KIKWETE‏


Na Anna Nkinda – Maelezo, Lindi
 Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kupitia wilaya ya Lindi mjini Mama Salma Kikwete amewaomba wananchi kuipigia kura ya ndiyo katiba inayopendekezwa kwa kuwa ni bora na imezingatia mahitaji ya makundi yote ya jamii.

Mama Kikwete ambaye ni Mke wa Rais Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete ametoa ombi hilo jana wakati akiongea na wananchi waliohudhuria mkutano wa hadhara uliofanyika  katika tawi la Mikumbi Magharibi  kata ya Wailes wilayani humo.

Alisema katiba inayopendekezwa ni ya watanzania wote na imegusa maeneo yote muhimu kwa ustawi wa wananchi, inazungumzia haki za wanawake, wazee, wavuvi, watoto na watu wenye mahitaji maalum.

“Katiba iliyopo sasa nayo ni bora,  lakini hii inayopendekezwa ni bora zaidi kwani imezitaja haki za mwanamke, mtoto, kijana,mzee na watu wenye  mahitaji maalum lakini katika  katiba hii ya sasa makundi haya hayatajwi. Msipoteze nafasi,  siku ikifika jitokezeni kwa wingi mkaipigie kura ya ndiyo”, Mama Kikwete alisema.

MNEC huyo pia aliwahimiza  wananchi hao kujitokeza  kwa wingi kujiandikisha katika daftari la kudumu la wapiga kura ili waweze kuipigia kura katiba inayopendekezwa na kushiriki katika uchaguzi mkuu utakaofanyika mwishoni mwa mwaka huu wa kumchagua Diwani, Mbunge na Rais.

Alisisitiza, “Zoezi hili la uandikishaji katika daftari la kudumu la wapiga kura ni jipya, hata kama unakitambulisho cha zamani ni lazima ukajiandikishe ili uweze kupata kitambulisho kipya kwakuwa hicho cha zamani hakitatumika tena”,.

Kuhusu maambuki ya Virusi Vya Ukimwi alisema ni tatizo na kuwasihi wananchi hao kujilinda  na kutoruhusu ugonjwa huo  usio na kinga wala tiba kuingia  ndani ya nyumba zao.

“Hali ya maambukizi ya ugonjwa wa Ukimwi katika nchi yetu inazidi kupungua kutoka asilimia 7.8 kwa mwaka 2005 hadi kufikia asilimia 5.1 kwa  mwaka 2014,  hadi sasa jumla ya wananchi milioni 24 wamepima  VVU kwa hiari.

“Kupima kwa hiari kutakusaidia kujua kama unamaambukizi au la, na ikiwa utakuwa na  maambukizi  utatumia dawa  za kupunguza makali ya ugonjwa na kuchukua tahadhari ili usiwaambukize wengine na kama hauna maambukizi utajikinga”, Mama Kikwete alisema.

Akiwasalimia wananchi waliohudhuria mkutano huo Mkuu wa Mkoa wa Lindi Mwantumu Mahiza aliwasisitiza wazazi na walezi kuona umuhimu wa kusimamia elimu ya  watoto wao kwani wakisoma wataweza kuzitumia fursa za kitaalam zinazopo mkoani humo.

Alisema hivi sasa shule za msingi na Sekondari ziko nyingi lakini cha kushangaza kuna baadhi ya wazazi hawataki kuwapeka watoto wao shule.

Mahiza alihimiza, “Kwa yeyote anayejijua ana mtoto nyumbani ambaye amefaulu mtihani wa darasa la saba na hataki kumpeleka  shule ajiandae kwakuwa  hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yake, natoa angalizo ifikapo ijumaa ya wiki hii watoto hawa wawe shuleni kwani elimu ni mkombozi wa maisha yao”, .

Katika mkutano huo  wanachama  wapya  202 walijiunga na Chama Cha Mapinduzi  kati ya hao wawili walitoka Chama cha Wananchi CUF.

Wakati huo huo MNEC Mama Kikwete  alitembelea kwa nyakati tofauti matawi ya Mmongo, Majani Mapana na Mikumbi Magharibi na kuongea na  viongozi wa Halmashauri kuu ya matawi mambo mbalimbali yahusuyo chama hicho .

Aliwataka wajumbe kuwahimiza wananchi wawe na  utamaduni wa kufuga kuku wa asili (kienyeji) kwa kila kaya kwa kufanya hivyo  itawasaidia kukuza uchumi wao na familia zao na hivyo kujikomboa kutoka maisha ya umaskini.

Mama Kikwete alisema ufugaji wa  kuku wa asili hauna gharama kwani kuku mwenyewe anajitafutia chakula,  mfugaji atakachompa ni mtama au pumba kidogo na maji ya kunywa pia nyama yake ni tamu na haina madhara kiafya ukilinganisha na kuku wa kisasa.

Alisema, “Ufugaji wa kuku una faida licha ya kuwa ni kitoweo bali pia ni biashara, hivi sasa kuku  mmoja anauzwa shilingi 12000 hadi 15000, ukiuza mmoja ada ya shule itapatikana na mtoto atasoma na wewe mwenyewe utavaa. Jitahidini kila kaya iwe na kuku japo 20”,.

Kwa upande wa ardhi aliwasisitiza kutokubali  kuuza maeneo yao kiholela kwani maeneo mengi yako karibu na Bahari ya Hindi na  thamani yake ni kubwa hivyo basi wayatunze yatawasaidia katika siku zijazo .

Mama Kikwete yupo wilayani humo kwa ajili ya kuimarisha kazi za CCM ikiwa ni pamoja na kufanya vikao na viongozi na kuangalia utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya mwaka 2010.
Mwisho.
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Lindi Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa