Na Anna Nkinda – Lindi
Wanachama wa
Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Lindi mjini wametakiwa kutokubali kurubuniwa
kwa kitu chochote kile ili wawapigie kura wagombea wa vyama vya upinzani bali waungane
kwa pamoja katika kampeni na kuhakikisha chama hicho kinapata ushindi wa
kishindo.
Mwito huo umetolewa
jana na Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya
Taifa (NEC) ya CCM kupitia wilaya ya Lindi mjini Mama Salma Kikwete wakati
akiwanadi kwa wananchi wagombea wa chama hicho wanaowania nafasi za uongozi kwenye
uchaguzi wa Wenyeviti na Wajumbe wa Serikali za Mitaa katika Kata ya Mwenge.
Mama Kikwete ambaye ni
Mke wa Rais Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete alisema lengo la chama chochote cha
Siasa ni kushika Dola kuanzia ngazi ya mtaa hadi Taifa hivyo basi wanachama hao wasikubali kurubuniwa bali
waendelee kukitetea na kukipigania Chama chao ili kipate ushindi katika mitaa yote 117 ya Kata hiyo.
“Viongozi wanaogombea
tena wamechaguliwa kutokana na kazi yao nzuri. Nanyi ambao kura zeu hazikutosha
wakati wa mchakato wa kuchagua msilaumu, bali muwapiganie wagombea wote na kuhakikisha wanashinda
angalieni maslahi ya chama kwanza mambo
binafsi baadaye”, alisema Mama Kikwete.
Aidha Mama Kikwete aliwaomba
wananchi wa wilaya hiyo kutumia maarifa na ujuzi waliopewa na Mwenyezi Mungu wa
kutambua mema na mabaya na kutokubali kudanganywa na kundi la watu wachache ili
waipoteze amani yao.
Mama Kikwete alisema, “Wenzenu
wamepiga hatua kubwa za maendeleo katika
mikoa yao huku Lindi Mwenyezi Mungu katupa neema maendeleo yanakuja sasa. Wanakuja
huku kuwadanganya ili mfanye vurugu na kurudisha maendeleo yenu nyumba, msifuate
mkumbo na kuchezea amani kwani vurugu
zinarudisha nyuma maendeleo”.
Aliwasihi wananchi
waliohudhuria mkutano huo kuhakikisha watoto wao wanaenda shule ili wapate
viongozi wazuri wa baadaye ambao watawaletea maendeleo kwani bila ya kuwa na
elimu ni vigumu kupata maendeleo.
MNEC huyo pia aliwashukuru
wanaume waliowaruhusu wake zao kugombea nafasi mbalimbali za uongozi na
kuwapongeza wanawake kwa kutokukubali kubaki nyuma na kuomba kugombea nafasi hizo.
Mama Kikwete yupo
wilayani humo kwa ajili ya shughuli za kichama ikiwa ni pamoja na
kushiriki kwenye kampeni na kuwanadi
wagombea wa chama hicho wanaowania nafasi mbalimbali za uongozi katika uchaguzi
wa viongozi wa Serikali za Mitaa, Vijiji na Vitongoji utakaofanyika tarehe 14 mwezi huu
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
0 comments:
Post a Comment