Home » » Mstahiki Meya Jerry Silaa awataka wakazi wa mkoa wa Lindi kujitokeza kwa wingi kujiandikisha katika daftari la kudumu la wapiga kura‏

Mstahiki Meya Jerry Silaa awataka wakazi wa mkoa wa Lindi kujitokeza kwa wingi kujiandikisha katika daftari la kudumu la wapiga kura‏


Na Anna Nkinda – Maelezo, Lindi
2/2/2015 Wakazi wa mkoa wa Lindi wametakiwa kujitokeza kwa wingi kujiandikisha katika daftari la kudumu la wapiga kura ili waweze kushiriki kwenye uchaguzi mkuu utakaofanyika mwishoni mwa mwaka huu.

Rai hiyo imetolewa jana na Mjumbe wa Kamati kuu ya Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM)  Jerry Silaa  wakati akiongea kwenye kilele cha sherehe za kutimiza miaka 38 ya chama hicho  mkoani Lindi zilizofanyika katika tawi la  Mnazi Mmoja lililopo kata ya Mingoyo wilaya ya  Lindi mjini.

Silaa mbaye pia ni Mstahiki Meya wa Manispaa ya Ilala alisema iwapo  mtu atajiandikisha katika daftari la kudumu la wapiga kura   atashiriki  katika uchaguzi mkuu ujao hivyo basi wakati ukifika ni jukumu la  mabalozi kuwahimiza  wananchi  kujiandikisha ili wasipoteze haki yao ya msingi ya kupiga kura.

Aidha Meya Silaa aliwapongeza  wana CCM kwa ushindi wa asilimia 77 walioupata wakati wa uchaguzi wa Serikali za mitaa, vijiji na vitongoji  uliofanyika mwishoni mwa mwaka jana na kuwataka kuwa makini katika kuteua viongozi wanaokubalika na wananchi  na kuachana na makundi yanayokibomoa chama hicho  kwa kufanya hivyo  itawawezesha  kupata ushindi  wa kishindo katika uchaguzi ujao.

Kwa upande wa vijana aliwahimiza kujishughulisha katika shughuli za kimaendeleo ili waweze kujipatia  maendeleo  kwani  mkoa wa Lindi uko katika dira ya maendeleo kwa kuwa na  ardhi yenye rutuba, barabara nzuri na gesi.

Silaa alisisitiza, “Nawashauri vijana wenzangu  mjiunge na  CCM chama kinachowasaidia vijana kuwaletea maendeleo ukilinganisha na vyama vingine vinavyowapotezea muda na kurudisha nyuma maendeleo yenu”.

Alikipatia kikundi cha ujarisiamali cha Zamira ambacho kinajishughulisha na shughuli za kilimo cha mikorosho, mihogo, karanga na kunde shilingi laki tano ili ziweze kuwasaidia kununua pembejeo za kilimo.

Naye  Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) kupitia wilaya ya Lindi mjini Mama Salma Kikwete alisema sherehe hizo zina umuhimu wa kipekee kwa wana CCM kwani zimeangukia mwaka wenye matukio muhimu na makubwa kwa nchi  ambayo ni kura ya maoni ya katiba inayopendekezwa na uchaguzi mkuu wa madiwani, wabunge na Rais.

Mama Kikwete ambaye ni Mke wa Rais Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete alisema  mwaka 2015 ni mwaka wa kuhitimisha utekelezaji wa Ilani ya CCM ya mwaka 2010-2015 ambapo Chama hicho kiliwaomba wananchi wakichague ili kiwafanyie kazi watanzania ambao walikiamini na kukichagua.

“Matokeo yake watanzania wameyaona , miundombinu ya barabara, shule na vyuo vimejengwa  na watoto wengi hivi sasa wapo mashuleni. Huduma za afya zimeboreka kwa kujengwa Hospitali, vituo vya afya na Zahanati”.

Lakini hata kwa yale ambayo hayakuwepo kwenye Ilani na yalikuwa ni matakwa ya wananchi chama chetu sikivu hakikusita kuyakubali kwani yalikuwa ni kwa ajili ya maslahi ya Taifa na vizazi vyetu”, alisema Mama Kikwete.

Kuhusu Katiba inayopendekezwa MNEC huyo alisema itapigiwa kura ya maoni mwaka huu mwezi wa nne hivyo basi aliwataka wanaCCM na watanzania wote kwa ujumla kuipigia kura ya ndiyo katiba pendekezwa kwani inakidhi matakwa ya watanzania kwa kuwa imegusa katika maeneo yote.

Akiwasalimia wananchi waliohudhuria sherehe hizo Mkuu wa wilaya ya Lindi Dkt. Nassoro Hamidi aliwahimiza wazazi kuhakikisha watoto walioandikishwa  darasa la kwanza na wale waliochaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza wanaenda shule kuanza masomo ili waweze kupata elimu itakayowasaidia  katika maisha yao.

Katika kilele cha sherehe hizo zilizoenda sambamba na wiki ya Chama na Jumuia zake kauli mbiu yake ni Umoja ni ushindi, Katiba yetu, Taifa letu  jumla ya wanachama wapya 448 walijiunga na chama hicho ambapo saba walitoka vyama vya upinzani,  Chama cha Wananchi (CUF) watano na Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) wawili.
Mwisho.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Lindi Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa